
Na Mwandishi Wetu
Musoma
--------------

Picha ya pamoja
Musoma
--------------
Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeendesha semina ya siku moja kwa waandishi wa habari wa mkoani Mara kuwajengea uelewa kuhusu majukumu ya mamlaka hiyo na mchango wake katika maendeleo ya sekta za nishati na maji nchini.
Semina hiyo imefanyika leo Jumanne, Juni 23, 2026, mjini Musoma, ambapo wanahabari hao wameelimishwa shughuli za EWURA na huduma zinazodhibitiwa na mamlaka hiyo.
Miongoni mwa mada zilizowasilishwa katika semina hiyo ni kazi na majukumu ya Ofisi ya EWURA Kanda ya Ziwa, uwekezaji wa vituo vya mafuta vijijini, wajibu wa EWURA katika utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia na jinsi inavyopokea na kutatua malalamiko na migogoro katika sekta zinazodhibitiwa na mamlaka hiyo.
Wawezeshaji wa mada hizo ni Meneja wa EWURA Kanda ya Ziwa, Mhandisi Nyirabu Musira, Mkaguzi wa Mafuta Kanda ya Ziwa, Atubele Byamungu na Ofisa Huduma kwa Wateja, Jesca Sewando.
Watoa mada hao walieleza kuwa EWURA inaendelea kusimamia kwa karibu utoaji wa huduma bora, salama na endelevu katika sekta za nishati na maji, huku ikihakikisha wananchi wanapata haki zao kupitia mifumo mbalimbali ya usimamizi na utatuzi wa migogoro.
Aidha, semina hiyo ilitoa fursa kwa waandishi wa habari kuuliza maswali, kutoa maoni na kupata ufafanuzi kuhusu changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika sekta hizo.

Picha ya pamoja
Akizungumza kwa niaba ya washiriki, Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Mara, Jacob Mugini, aliwashukuru wawezeshaji kwa semina hiyo, akisema imewawezesha kuelewa kwa undani masuala ya udhibiti wa huduma za nishati na maji.
Mugini amesema maarifa waliyoyapata katika semina hiyo yatawawezesha kuandika habari sahihi kuhusu EWURA na zenye manufaa kwa wananchi.
“Tunawashukuru kwa mafunzo haya muhimu, tunawaahidi kwamba tutakuwa mabalozi wazuri wa EWURA kupitia kalamu zetu kwa kuhabarisha umma kuhusu majukumu, huduma ya mamlaka hii,” alisema Mugini.
Naye mwandishi wa habari kutoka Mara Online News, Christopher Gamaina, amesema semina hiyo ni hatua muhimu ya kuimarisha ushirikiano kati ya EWURA na wanahabari na kuhakikisha umma unapata taarifa sahihi kuhusu huduma zinazodhibitiwa na mamlaka hiyo kwa maendeleo ya jamii na taifa.
No comments:
Post a Comment