NEWS

Saturday 26 October 2019

MARA ONLINE WAUNGA MKONO JUHUDI ZA SERIKALI KUBORESHA ELIMU TARIME



Na mwandishi wetu, Tarime
 Mtendaji Mkuu wa Mara Online(CEO) Jacob Mugini ametoa wito kwa wanafunzi wanaonufaika na mpango wa elimu bila malipo kusoma kwa bidii kama namna bora ya kuishukuru serikali.
Mugini alitoa wito huo hivi karibuni katika mahafali ya 12 ya kadato cha nne katika shule ya sekondari Nkende iliyopo Halmashauri ya Mji wa Tarime Mkoani Mara.
“ Sisi wakati tunasoma hatukuwahi bahatika kupata elimu bure, ulikuwa unafanya mtihani unafikiria  utatoa wapi karo. Elimu bure ni fursa nzuri kwenu  na kwa namna ya kipekee napenda kutumia fursa hii kuishukuru serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi wa Rais  wetu Mhe Dkt John Magufuli kwa  kutoa elimu bure  kwa vijana ambao wanahitimu leo hapa Nkende sekondari“, Mugini ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika  mahafali hayo alisema.

“ Ninyi mnabahati kubwa ya  kuwa matunda ya kwanza ya elimu bure kwa upande wa sekondari , hivyo namna bora ya kuonesha shukurani ni kufaulu mitihani yenu kwa alama za juu”,  Mugini ambaye kitaaluma ni mwandishi wa habari aliwaasa watahiniwa 159 wa kidato cha nne katika mahafali ya 12 ya shule hiyo.

Katika risala yao kwa mgeni rasmi, watahiniwa  wa shule walitumia fursa hiyo kumshukuru Rais Magufuli na serikali  kwa kutoa elimu bila malipo.
“ Hakika mpango wa elimu bure umekuwa msaada mkubwa sana kwetu na wazazi ambao wengi wao wana kipato cha chini “, ilisema sehemu ya risala ya wanafunzi hao.

 Mugini pia  alikabidhi msaada wa Kompyuta Mpakato (laptop) mbili kwa ajili ya kuboresha utoaji wa elimu katika shule hiyo ambayo ipo  katika Halmashauri ya Mji wa Tarime Mkoani Mara.
“ Sisi kama Mara Online tunafurahi kuwapatia  hizi laptop mbili ili kutatua sehemu ya changamoto zilizopo katika shule hii yenye walimu wazuri na wanafunzi wazuri “, alisema Mugini.

Mwanahabari huyo ambaye amejikita katika habari za maendeleo na uhifadhi wa mazingira  alitoa wito kwa wazazi kutimiza wajibu wao ili kuwasaidia watoto wao kufikia ndoto zao kielimu bila kubagua watoto wakike.
“ Wapeni pia watoto wakike fursa ya kupata elimu.Msiwafanye kama wafanyakazi wa ndani . Na pia kuna tabia mbaya ya wazazi kuwatumia wanafunzi kuchunga ng’ombe baadala ya kuwapatia muda wa kutosha kujisomea”, alisema Mugini. 


Mara Online pia walitoa zawadi kwa wanafunzi wa kidato cha nne saba ambao wamekuwa wakifanya vizuri kitaaluma katika shule hiyo.
Mkuu wa shule ya Nkende sekondari Samson Hagai alimshukuru pia Rais Dkt.John Magufuli   na  serikali ya awamu ya tano  kwa kuendelea kutoa fedha kila mwezi kwa ajili ya kuendesha shule hiyo ambayo ina zaidi ya wanafunzi 800 wanaonufaika na elimu bila malipo.
Hagai alisema  msaada wa laptop uliotolewa na Mara Online  utaboresha utendaji kazi wa walimu  na hivyo kuongeza ufanisi katika shule hiyo.
“ Laptop mbili hizi zitatusaidia katika shughuli mbalimbali za kitaaluma ikiwemo usajili wa wanafunzi wa kidato cha pili na cha nne katika mfumo uliotolewa na baraza la mitahani”, alisema Hagai

 Kwa upande wake Makamu Mkuu wa shule hiyo Chacha Nchagwa alisema msaada   huo uliotolewa na Mara Online umetatua moja ya changamoto kubwa ya shule hiyo  ambayo ni moja ya shule za kata zilizofunguliwa mwaka 2005.

1 comment:

  1. Mungu awabariki sana kwa msaada mlioutoa. Endeleani kutenda hivyo na kwa wengine pia.

    ReplyDelete

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages