NEWS

Tuesday 2 June 2020

Tausi wa Mama Maria watua Butiama, Madaraka Nyerere anena


TAUSI ambao Rais Dkt John Magufuli alimpatia mjane wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Mama Maria Nyerere, wamewasili salama nyumbani kwa mama huyo Mwitongo, Butiama mkoani Mara.
Tausi waliotolewa na Rais Dkt John Magufuli kwa mjane wa Baba wa Taifa, Mama Maria Nyerere wakiwa kwenye banda baada ya kupokewa na familia ya Mwalimu Julius Nyerere katika bustani ya eneo la Mwitongo, Butiama.
Akizungumza kwa niaba ya Mama Maria Nyerere, mtoto wa Baba wa Taifa, Madaraka Nyerere, amewambia waandishi wa habari nyumbani hapo leo Juni 2, 2020 kwamba ndege hao walipokewa Mwitongo Jumapili Mei 31, 2020 kutoka kwa Dkt Gabriel Nyanda wa Ikulu.

Itakumbukwa kwamba Jumamosi Mei 30, 2020 katika Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma, Rais Magufuli alimzawadia Mama Maria Nyerere tausi 25, sambamba na marais wastaafu, Ali Hasan Mwinyi, Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete ambao pia walizawadiwa kila mmoja tausi 25 kwa ajili ya kupendezesha bustani zao.
Mtoto wa Baba wa Taifa, Madaraka Nyerere akizungumza na wanahabari (hawapo pichani) kuhusu tausi waliopokewa Mwitongo

“Nawasilisha shukurani za dhati kwa Rais Dkt John Pombe Joseph Magufuli kwa uamuzi wake wa kutoa zawadi ya tausi 25 kwake Mama Maria. Narudia salamu za shukurani za Mama Maria, familia ya Mwalimu Nyerere na ukoo wa Mtemi Nyerere Burito kwa Rais Magufuli kwa kutoa zawadi hii kubwa na kuwezesha eneo hili la Mwitongo kuendelea kuboresha historia ya Mwalimu Nyerere,” amesema Madaraka.
 Kwa mujibu wa Madaraka, Mama Maria Nyerere anaamini tausi hao ni kielelezo cha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliozaa jina la Tanzania, kutokana na tausi wa kwanza kupokewa na Mwalimu Nyerere kutoka kwa Rais Aboud Jumbe wa Zanzibar.

Katika hatua nyingine, Madaraka ametangaza kufunguliwa kwa mapokezi ya watalii katika eneo la Mwitongo lililokuwa limefungwa tangu Aprili 2020 kwa ajili ya kuchukua tahadhari dhidi ya kuenea kwa maambukizi ya virusi vya corona (COVID 19).


“Sasa hivi eneo hili limefunguliwa tena na tunawakaribisha wageni kuja kujifunza machache juu ya historia ya Mwalimu Nyerere na kushuhudia zawadi ya tausi iliyotolewa na Mheshimiwa Rais,” amesema mtoto huyo wa Baba wa Taifa.

Madaraka amesema wanaendelea kuzingatia tahadhari zinazotolewa na wizara ya afya katika kuzuia maambukizi ya COVID 19 na amewaomba wageni watakaozuru eneo hilo kuvaa barakoa.

(Imeandikwa na Christopher Gamaina, Butiama)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages