NEWS

Monday 20 November 2023

Chandi atunukiwa cheti kwa uchapaji kazi, amshukuru Rais Samia kuelekeza fedha nyingi za miradi mkoani Mara, akiombea Chama ushindi mnono Uchaguzi wa Serikali za Mitaa



Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Musoma Mjini, Benedictor Maregesi (kulia) akimkabidhi Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Patrick Chandi cheti cha pongezi, jana Jumatatu.
--------------------------------------------------------

Na Godfrey Marwa, Musoma
Mara Online News
--------------------------------

CHAMA cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Musoma Mjini kimemtunuku Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Patrick Chandi cheti cha pongezi kwa kuchaguliwa kwa kishindo, pamoja na kazi nzuri anazoendelea kufanya kuimarisha chama hicho na jumuiya zake mkoani.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Musoma Mjini, Benedictor Maregesi alimkabidhi Chandi cheti hicho katika mkutano wa Halmashauri Kuu ya chama hicho wilayani humo, jana Jumatatu.

Chandi pia alipata fursa ya kusikiliza kero za wanachama na wananchi mbalimbali zikiwemo za uvuvi haramu katika Ziwa Victoria, migogoro ya ardhi, kikokotoo kisicho rafiki kwa watumishi, kadi za bima ya afya kutothamiwa, mama wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano kutotibiwa bure kama Ilani ya CCM inavyoelekeza, kisha akatatua baadhi na nyingine kuzitolea maelekezo ya kuzitafutia uvumbuzi.

Mwenyekiti Chandi akimpatia mjasiriamali na mkazi wa Musoma Mjini msaada wa mtaji wa biashara.
Aidha, Chandi alitumia nafasi hiyo pia kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa CCM Taifa, Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuelekeza fedha nyingi mkoani Mara kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo Hospitali ya Rufaa Kwangwa.

Aliwaomba wananchi kukipatia CCM ushindi mnono katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika mwakani, akisema ndicho chama kilichopewa dhamana kubwa ya kuhakikisha maendeleo ya kisekta yanapatikana nchi nzima.

“Mwakani tuna Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, naomba tukipe CCM ridhaa kwa kura nyingi kiendelee kushika dola na kuongoza Serikali kwa maendeleo ya Watanzania kwa ujumla,” alisema Chandi.

Chandi akisalimiana na wanachama wa CCM alipowasili Musoma Mjini, jana Jumatatu.
Mwenyekiti huyo wa CCM Mkoa wa Mara anaendelea na ziara yake ya kuimarisha Chama, kukagua maendeleo na kusikiliza kero za wananchi, akifuatana na wajumbe wa Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages