NEWS

Sunday 20 September 2020

Waziri Mkuu ampamba Waitara Tarime Vijijini

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimwombea kura mgombea ubunge jimbo la Tarime Vijijini kupitia CCM, Mwita Waitara kwa wananchi wa jimbo hilo (hawapo pichani) aliposimama kuzungumza nao eneo la Nyamwaga leo.

 

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amewaomba wakazi wa jimbo la Tarime Vijijini kuhakikisha wanamchagua mgombea ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CCM, Mwita Waitara, akisema ndiye suluhisho thabiti la matatizo yanayowanyima maendeleo ya kweli.

 

“Waitara ni kijana mchapa kazi, ameweza kufanya mambo mengi kwa maendeleo ya wananchi kupitia nafasi ya naibu waziri [wa Tamisemi], mchague huyu atakuwa msaada mkubwa kwenu wana-Tarime Vijijini.

 

“Mchagueni Waitara maana ana uwezo wa kuingia kwa rais moja kwa moja bila hodi, ataingia kwangu [Waziri Mkuu] na kwa waziri yeyote bila hodi kuwasilisha changamoto zenu na kuwaombea miradi ya maendeleo,” amesisitiza Majaliwa aliposimama barabarani kuzungumza na wananchi eneo la Nyamongo na baadaye Nyamwaga na mjini Tarime, leo Septemba 20, 2020.

Mgombea ubunge jimbo la Tarime Vijijini kwa tiketi ya CCM, Mwita Waitara (mwenye mic katikati) akizungumza katika mkutano wa wananchi uliohutubiwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa eneo la Nyamwaga leo.

 

Majaliwa amefafanua kuwa wakazi wa jimbo la Tarime Vijijini wakimchagua Waitara atashirikiana na Rais na yeye mwenyewe (Waziri Mkuu) kuharakisha ufumbuzi wa matatizo yanayowakabili yakiwamo ya malipo ya fidia kwa waliohamishwa kupisha mgodi wa dhahabu wa North Mara na upatikanaji wa ajira za wazawa katika mgodi huo.

 

Pia Waiatala atasaidia upatikanaji wa maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria, kupandisha hadhi eneo la Nyamongo kuwa mamlaka ya mji, ujenzi wa barabara ya lami ya Tarime – Nyamwaga hadi wilayani Serengeti, kurejesha mpango wa mgodi kugharimia mahitaji ya wanafunzi wa sekondari na vyuo, kuboresha huduma za afya na elimu, miongoni mwa huduma nyingine za kijamii na kiuchumi.

Wananchi wakishangilia katika mkutano wa kampeni ya kuwanadi wagombea ubunge kwa tiketi ya CCM, Michael Kembaki (Tarime Mjini), Mwita Waitara (Tarime Vijijini) na wagombea udiwani, uliohutubiwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kwenye viwanja vya soko la zamani la Tarime leo


Waziri Mkuu ametumia nafasi hiyo pia kuwaomba wakazi wa jimbo la Tarime Vijijini kumchagua mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dkt John Pombe Magufuli na wagombea udiwani katika kata mbalimbali jimboni humo wanaotokana na chama hicho.

 

Amefafanua kuhusu umuhimu wa kuchagua rais, wabunge na madiwani wanaotokana na CCM kuwa ni kuunda jopo la viongozi watakaozungumza lugha moja inayolenga kuwaletea wananchi maendeleo endelevu.

Mgombea ubunge jimbo la Tarime Vijijini kwa tiketi ya CCM, Mwita Waitara (kushoto) akizungumza katika mkutano wa kampeni uliohutubiwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa (kulia aliyesimama) kwenye viwanja vya soko la zamani la Tarime leo.


Naye Waitara ameahidi akipewa ridhaa ya kuwa mbunge wangusha wananchi wa jimbo la Tarime Vijijini akisema atatumia muda mwingi kuwasumbua Rais, Waziri Mkuu na viongozi wa wizara mbalimbali kwa ajili ya kuwaletea maendeleo ya kisekta.

 

(Habari na picha zote na Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages