NEWS

Wednesday 26 May 2021

Vijiji vyote kufikiwa na TASAF wilayani Itilima



Mkuu wa Wilaya ya Itilima Benson Kilangi akifungua kikao kazi

ZAIDI ya kaya 13,292 zilizopo kwenye vijiji 36 wilayani Itilima katika mkoa wa Simiyu zinatarajiwa kufikiwa na Mfuko wa Mendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF) awamu ya tatu wa kusaidia kaya maskini.

Hayo yamesemwa na Mratibu wa TASAF Wilaya ya Itilima, Eva Luchagula kwenye kikao kazi cha kujenga uelewa kuhusu sehemu ya pili ya awamu ya tatu ya TASAF kwa viongozi, watendaji na wawezeshaji kilichofanyika leo kwenye ukumbi wa halmashauri ya wilaya hiyo.

“Awali TASAF ilifikia vijiji 66 na hatua ya sasa itawezesha kufikia vijiji vyote 102 wilayani hapa,” alisema Luchagula.

Kwaupande wake, Afisa Ufatiliaji kutoka TASAF, Paulo Tibabihilila amesema wamejipanga kuhakikisha kaya zote zenye walengwa wilayani hapo zinafikiwa kwa kuzingatia vigezo na pasiwepo udanganyifu wa aina yoyote.

Aidha, mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF na Msimamizi wa shughuli ya utambuzi na uandikishaji wa kaya maskini wilaya ya Itilima, Emmanuel Luhanzo amesema takwimu zinaonesha umaskini na mahitaji ya msingi umepungua kwa asilimia 10.


Emmanuel Luhanzo mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF na msimamizi wa zoezi la utambuzi na uandikishaji wa kaya maskini wilaya ya Itilima

“Takwimu unaonyesha kuwa umasikini wa mahitaji ya msingi umepungua kwa asilimia 10 huku umaskini uliokithiri ukipungua kwa asilimia 12 kwa kaya hizo”alisema Luhanzo.

Aliongeza kuwa kipindi cha pili cha awamu ya tatu ya TASAF kitafikia kaya milioni 1,450,000 zenye jumla ya watu zaidi ya milioni saba nchini.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Benson Kilangi amesema watakaotambulika lazima wawe wamekidhi vigezo na elimu kwa walengwa itolewe mara kwa mara na waelimishaji wa TASAF ngazi ya jamii wakifanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia viapo vyao.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Elizabeth Gumbo amesema vijiji 36 vitatembelewa lengo likiwa kuibua kaya maskini ili malalamiko yaliyotokea kipindi cha nyuma yasiwepo tena.


Washiriki wa kikao kazi

(Habari na picha: Anita Balingilaki, Itilima)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages