NEWS

Tuesday 28 September 2021

Harambee ya ujenzi Kanisa Katoliki Masurura: Mbunge Ghati achangia laki 8, Paroko amshukuru




MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Mara, Ghati Zephania Chomete (pichani juu), ameshiriki harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa Katoliki (RC) Kigango cha Masurura, Parokia ya Kiagata wilayani Butiama.

Katika harambee hiyo iliyofanyika Jumapili iliyopita, Mbunge Ghati amechangia ujenzi huo fedha taslimu shilingi zaidi ya 800,000.

Akizungumza mbele ya waumini wa kanisa hilo, Mbunge huyo amemshuskuru Mungu kwa uponyaji aliompatia, baada ya kupata ajali ya gari miezi michache iliyopita.

Amesema anatambua mchango mbubwa unaofanywa na viongozi wa dini katika kudumisha upendo na amani nchini.

Mbunge Ghati (kulia) akitoa neno la shukrani wakati wa harambee hiyo. Kushoto ni Paroko wa Parokia ya Kiagata, Padre Faustine Abala.

Kwa upande wake, Paroko wa Parokia ya Kiagata, Padre Faustine Abala amemshukuru Mbunge Ghati kwa mchango huo.

“Tunaomba Mungu aendelee kumponya Mbunge Ghati, anafanya kazi nzuri ya kusaidia jamii na tunamtakia maisha mema na Mungu amsaidie kuwa na mafanikio katika shuguli zake za kibunge,” Paroko Abala ameiambia Mara Online News, baada ya halfa ya hiyo.

Paroko Abala ametumia nafasi hiyo pia kuhimiza jamii kuendelea kuchangia ujenzi wa makanisa, ili watu wapate nyumba za ibada, jambo ambalo pia litasadia kupunguza matendo maovu katika jamii.

Makundi mbalimbali ya wananchi wa mkoa wa Mara, wakiwemo wanachama wa Jumuiya ya CCM ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), yamekuwa yakimtembelea Mbunge Ghati nyumbani kwake mjini Musoma, kumjulia hali na kumpa pole yeye na mume wake, Marwa Mathayo, kutokana na ajali ya gari waliyopata miezi michache iliyopita.


(Imeandikwa na Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages