NEWS

Tuesday 14 September 2021

Ujerumani yaipiga jeki Tanzania kwa bilioni 68 kuimarisha uhifadhi



TANZANIA na Ujerumani zimesaini mikata mitatu kuhusu Sh bilioni 68 zitakazotolewa na Serikali ya Ujerumani, kwa ajili ya kuimarisha uhifadhi katika Hifadhi za Taifa za Serengeti, Katavi na Mahale.

Tukio hilo limefanyika leo Septemba 14, 2021 katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, ambapo Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW), Jennifer Woerl amehusika kusaini mikataba hiyo.


Jennifer Woerl (wa pili kushoto) akisaini mkataba

Kwa Upande wa Tanzania, waliowakilisha Serikali kusaini mikataba hiyo ni Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Jenerali (Mstaafu) George Waitara na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt Allan Kijazi.


Dkt Kijazi (kushoto) akisaini mkataba

Viongozi hao wamesaini mikataba hiyo mbele ya Mkurugenzi wa Masuala ya Afrika Kutoka Serikali ya Ujerumani, Dkt Stefan Oswald na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja, miongoni mwa viongozi wengine.

Dkt Oswald na Woerl wamesema Ujerumani imetoa msaada wa fedha hizo kutokana na kuridhishwa na jitihada zinazofanywa na Serikali ya Tanzania katika uhifadhi wa wanyamapori.

Dkt Oswald ameongeza kuwa msaada huo ni sehemu ya kuendeleza uhusiano na urafiki wa muda mrefu wa miaka 60 sasa baina yake na Tanzania, ulioasisiwa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na Mkurugenzi wa zamani wa Shirika la Uhifadhi la Frankfurt Zoological Society (FZS) la Ujerumani, Profesa Bernhard Grzimek.

Naibu Waziri Masanja ameishukuru Serikali ya Ujerumani akisema fedha hizo zitasaidia kuimarisha shughuli za uhifadhi wa mifumo ya ikolojia katika hifadhi husika.

Kuhusu mfumo wa ikolojia ya hifadhi za Katavi na Mahale, Dkt Kijazi amesema “Idadi kubwa ya soko wanatumia eneo linalounganisha linalounganisha hifadhi hizi, hivyo msaada huu utasaidia kushirikisha jamii kulinda ikolojia ya ushoroba huo.”

Kwa upande wake, Jenerali Waitara aamesema fedha hizo zitasaidia pia kuboresha miundombinu katika hifadhi hizo na uendeshaji wa TANAPA.

(Habari na picha zote: Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages