NEWS

Monday 29 November 2021

AICT Mara na Ukerewe yahamasisha ujumuishaji watoto wenye ulemavu kupata elimu bora



KANISA la AICT Dayosisi ya Mara na Ukerewe kwa kushirikiana na taasisi ya Right to Play, limehamasisha jamii kujumuisha watoto wenye ulemavu katika kupata elimu bora.

Uhamasishaji huo umefanyika baada ya mashindano ya michezo mbalimbali kwa wanafunzi wa darasa la kwanza hadi la nne wa shule za Msingi Nyamwaga na Maika zilizopo kata ya Nyamwaga wilayani Tarime, yaliyofanyika leo Novemba 29, 2021.



“Lengo kubwa katika hii michezo ni kuhamasisha kupata elimu iliyo bora kwa watoto wote, wakiwemo na watoto wenye ulemavu, au mahitaji maalumu na tuwapende kama watoto wengine bila kuwanyanyapaa,” Afisa Mradi wa Kanisa hilo, Rebeca Bugota amesema.


Rebeca akizungumza

Rebeca amesisitiza kuwa jamii yote ina wajibu wa kuhakikisha watoto wenye mahitaji maalumu wanajumuishwa katika kupata elimu, ikiwa ni pamoja na kubaini na kushughulikia vikwazo vya kielimu vinavyowakabili watoto hao, ili kuwezeshwa kwenye ujifunzaji bora, kwani ulemavu siyo ugonjwa.

Ameweka wazi kuwa mradi huo unawalenga wanafunzi wa darasa la awali, la kwanza hadi la nne, ukijumuisha walimu, jamii na wadau wa elimu kwa ujumla.



Naye Mwalimu David Daniel wa Shule ya Msingi Nyamwaga ambaye ni mlemavu wa macho, amelishukuru Kanisa la AICT na taasisi ya Right to Play kwa kupaza sauti juu ya watoto wenye ulemavu, maana imewafanya wajione wana umuhimu katika jamii.

“Ninachoamini ni kwamba watoto wote, wakiwemo walemavu wana haki ya kusoma kama watoto wengine na hata wana uwezo wa kupata nafasi ya uongozi, ukiwemo urasi,” Mwalimu Daniel amesema.

Katika mashindano yaliyofanyika, Shule ya Msingi Maika imeibuka kidedea kwenye mchezo wa mpira wa miguu, huku Shule ya Msingi Nyamwaga nayo ikijinyakulia ushindi kwenye mpira wa pete.

(Imeandikwa na Goefrey John wa Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages