NEWS

Tuesday 14 June 2022

Halmashauri Serengeti wamshukuru Rais Samia kuwapa mabilioni ya fedha za maendeleo, Makuruma awapongeza Mbunge Dkt Amsabi na DC Mashinji kwa uchapaji kazi


HALMASHAURI ya Wilaya ya Serengeti imeishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan (pichani juu), kwa kutoa shilingi zaidi ya bilioni saba kugharimia miradi mbalimbali ya maendeleo.

“Pamoja na miradi mingi ambayo Mheshimiwa Rais Samia ametupatia, kuna shilingi zaidi ya bilioni saba zimengia kwenye halmashauri yetu kwa ajili ya maedeleo. Jambo jema lazima lisemwe,” Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti, Ayub Mwita Makuruma (pichani juu kulia) amesema wakati akiahirisha kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo mjini Mugumu, hivi karibuni.
Mwenyekiti Makuruma (kulia) na Mkurugenzi Mtendaji, Kivuna Msangi kikaoni

Kauli hiyo ya Makuruma ilifuatiwa na mwitikio wa madiwani na viongozi wengine, wakiwemo Mbunge wa wa Serengeti, Dkt Amsai Mrimi na Mkuu wa Wilaya (DC) hiyo, Dkt Vincent Mashinji, ambao walipiga makofi kuashiria kumshukuru Rais Samia kutokana na fedha hizo za kugharimia miradi mbalimbali, ikiwemo ya elimu, afya, maji na barabara.

Makuruma amempongeza pia Mbunge Dkt Amsabi kwa kazi nzuri ya kutekeleza ahadi zake zinazolenga kuleta mageuzi ya maendeleo ya kisekta katika jimbo hilo.

“Hii kazi nzuri ya Rais wetu ya kuiletea maendeleo wilaya yetu inafanywa sambamba na mbunge wetu wa jimbo la Serengeti,” amesema Makuruma ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Busawe kwa tiketi ya chama tawala - CCM.

Mwenyekiti huyo wa Halmashauri amewaomba madiwani na wana-Serengeti kwa ujumla kuendelea kumpa ushirikiano Mbunge huyo ili kuharakisha maendeleo yao ya kijamii na kiuchumi.
Mbunge Dkt Amsabi akiuliz swli bungeni

Hata hivyo, Makuruma amewakemea watu wanaotumia muda mwingi kukosoa utendaji wa Mbunge Amsabi kwenye mitandao ya kijamii, badala ya kumpa ushirikiano.

“Huwa nawashangaa wanaombeza, ee mbunge amefanya nini,” Makuruma amesema akionekana kukerwa na wakosoaji hao akisisitiza kuwa wanapaswa kuona mababiliko ya kimaendelea yaliyoanza kuonekana jimboni.

Amesema ni vigumu kutenganisha maendeleo yanayofanyika katika jimbo la Serengeti na juhudi zinazofanywa na Mbunge Amsabi za kutekeleza ahadi zake.

Mwenyekiti huyo amemhakikishia Dkt Amsabi ushirikiano wa kutosha, huku akituma salamu kwa wanaomezea mate kiti cha ubunge wa Serengeti kutafuta kazi ya kufanya.

“Kwa sasa hivi mtu kusema maneno kwenye mitandao ni jambo la kushangaza sana, wasubiri miaka mitano. Tupo pamoja, nakuhakikishia kuwa utarudi tena,” amesema Makuruma - akimaanisha kuwa Dkt Amsabi atachaguliwa tena katika uchaguzi mkuu mwaka 2025.
Madiwani kikaoni

Amewataka madiwani wa halmashauri hiyo kuyasemea mambo mazuri yanayofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita kwa kushirikiana na Mbunge Amsabi katika kuwaletea wananchi maendeleo.

Makuruma amemmiminia sifa DC Mashinji, akisemai ni kiongozi mwenye maono mazuri katika kupaisha maendeleo ya kisekta wilayani Serengeti.
DC Dkt Mashinji

“DC unafanya kazi nzuri na maombi yetu ni kwamba uendelea kuwa Serengeti,” Makuruma amesema huku akijivunia pia ushirikiano ulipo kati ya ofisi yake, DC Mashinji na Mbunge Amsabi.

Ahueni baada ya UVIKO
Katika hatua nyingine, Makurujma amesema halmashauri hiyo imeanza kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, baada ya kupitia kipindu kigumu cha mlipuko wa janga la UVIKO-19.

Amesema tayari hamashauri hiyo imetoa Sh milioni 400 kughamiria miradi ya maendeleo ya wananchi katika mwaka huu wa fedha (2021/2022) kutokana na mapato ya ndani.

“Kitakwimu tupo vizuri kwenye mapato ya ndani kwa sasa. Shilingi milioni 400 zimepelekwa kwenye miradi ya maendeleo,” alisema Makuruma.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo, halmashauti hiyo ilikuwa haifanyi vizuri kwenye ukusanyaji mapato na kwamba hali ilikuwa mbaya zaidi kipindi cha UVIKO-19.

“Watu wanasahau tulikotoka, kipindi cha nyuma hakuna fedha ilikuwa inaenda kwenye miradi kutoka kwenye asilimia 40, mapato yalikuwa yanapotea,” amesema Makuruma, huku akimpongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Kivuna Msangi kwa kusimamia vizuri suala la utendaji.

Ameongeza kuwa hata fedha za vikundi vya wanawake, vijana na wenye lemavu, sasa zimeanza kutolewa na halmashauri hiyo bila kikwazo.

Matunda ya Royal Tour
Makuruma pia amesema ujio wa Filamu ya Royal Tour utasadia kuongeza mapato ya ndani ya halmashauri hiyo kutokana na kodi zinazolipwa na wawekezaji katika sekta ya utalii wilayani Serengeti.

Amesema watalii wameanza kumiminika kwenye hoteli na kambi za kitalii zilizopo wilayani Serengeti mara baada ya uzinduzi wa filamu hiyo.

“Ripoti inaonesha hali ilikuwa mbaya sana, lakini sasa kuna taarifa njema kuwa wageni wameanza kuwa wengi katika hoteli na camps (kambi) zilizopo Serengeti, baada kuzinduliwa kwa Filamu ya Royal Tour,” Makuruma amesema huku akimpongeza tena Rais Samia kwa kuwapa Watanzania zawadi ya filamu hiyo.

Hivyo amewahimiza madiwani wa halmashuri hiyo kuendelea kuisemea Serikali mambo mazuri inayofanya kwa wananchi na kuwatumikia kwa moyo mkunjufu, ili iweze kusonga mbele kimaendeleo.

“Serengeti ni yetu sote, tuitumikie kwa moyo mmoja,” alisisitza Makuruma.

Awali, Mweka Hazina mpya wa Halmashauri hiyo, Saad Ishabailu alijitambulisha katika kikao hicho na kuwaomba madiwani ushirikiano, hasa wa kumsaidia kwenye ukusanyaji wa mapato, ili kufanikisha utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya wananchi.

(Imeandikwa na Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages