NEWS

Saturday 4 February 2023

Rais Samia atuma salamu za rambirambi vifo vya watu 17 waliopoteza maisha katika ajali ya magari Tanga



Na Mwandishi Wetu
---------------------------------

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan (pichani), ametuma salamu za rambirambi - akieleza kusikitishwa na tukio la watu 17 walioripotiwa kupoteza maisha katika ajali ya magari wilayani Korogwe, Tanga.

“Nimesikitishwa na vifo vya watu 17 vilivyosababishwa na ajali iliyotokea jana saa 4:30 usiku eneo la Magila Gereza, wilaya ya Korogwe, mkoa wa Tanga. Nawapa pole wafiwa na wote walioguswa na vifo hivi. Nawaombea ndugu zetu hawa wapumzike mahali pema na majeruhi wapone haraka,” Rais Samia ameandika katika ukurasa wake wa Twitter leo asuhuhi.

Taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Omary Mgumba leo na kuanza kuripotiwa na Mwananchi, imesema pia watu 12 walijeruhiwa katika ajali hiyo iliyotokea katika barabara ya Segera - Buiko eneo la Magira Gereza.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, magari yaliyohusika ni aina ya Mitsubishi Fuso na Coaster iliyokuwa imebeba mwili wa marehemu na abiria 26 ikitokea Dar es Salaam kwenda Moshi, Kilimanjaro kwenye mazishi.

“Ajali hii imesababisha vifo 17 na majeruhi 12 ambao majina yao hayajafahamika, miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali yetu ya Wilaya ya Korogwe, majeruhi 10 wamehamishiwa Hospitali ya Mkoa wa Tanga, Bombo na majeruhi wawili wamebaki Hospitali ya Korogwe,” imeeleza taarifa hiyo.

Chanjo cha ajali hiyo kimetajwa kuwa ni mwendo kasi na uzembe wa dereva wa Fuso kulipita gari la mbele bila ya kuchukua tahadhari na kugongana na Coaster.

1 comment:

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages