NEWS

Sunday 30 July 2023

WAMACU wawashushia wakulima tani 31 za mbegu bora za mahindi kutoka Bayer Life Science Tanzania Limited


Na Mwandishi wa

Mara Online News

---------------------------

 CHAMA Kikuu cha Ushirika cha Wakulima wa Mara (WAMACU Ltd) kimeshusha tani 31 (sawa na kilo 31,000) za mbegu bora za mahindi aina ya DK kutoka Kampuni ya Bayer Life Science Tanzania Limited, kwa ajili ya kuuzia wakulima kwa bei nafuu.


 Mara Online News ilishuhudia mbegu hizo zikishushwa kwenye maghala ya WAMACU Ltd yaliyopo eneo la Rebu mjini Tarime, jana.


 Kwa mujibu wa Meneja Mkuu (GM) wa WAMACU Ltd, Samwel Gisiboye, mbegu hizo zitauzwa kwa bei ya shilingi 14,000 kwa mfuko wa kilo mbili kipindi hiki cha msimu wa vuli.


 “Tumeamua kuwaletea wakulima mbegu hizi ili kuwaepusha kununua zinazotoka nje ya nchi ambazo mara nyingi zinachakachuliwa na kuwaingiza wakulima hasara.


 “Hivyo tunawahimiza wakulima wetu kutumia mbegu hizi ambazo hutengenezwa hapa nchini na Kampuni ya Bayer  iliyoidhinishwa na Serikali yetu,” alisema GM Gisiboye katika mazungumzo na Mara Online News ofisini kwake, jana.

 Alisema WAMACU Ltd itaendelea kuongeza mbegu nyingi iwezekanavyo ili kutosheleza mahitaji ya wakulima. “Tunatarajia kuongeza mbegu hizi hadi kilo 150,000 msimu huu wa vuli,” alisema.


 Kwa mujibu wa Kampuni ya Bayer Life Science Tanzania Limited, mbegu bora za mahindi aina ya DK huzaa mapema, punje zake ni kubwa, hukomaa ndani ya siku 90 hadi 110 na mavuno yake ni magunia 28 hadi 32 kwa ekari moja.

 

#Tunakuhabarisha Ukweli kwa Weledi

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages