NEWS

Saturday 9 May 2020

Wanaouza sukari bei juu Bariadi sasa kukiona



SERIKALI wilayani Bariadi katika mkoa wa Simiyu, imejipanga kuanza operesheni ya kuwasaka wafanyabiashara wanaouza sukari kwa bei ya juu, kinyume cha bei elekezi iliyotangazwa na Serikali kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara.

Hatua hiyo imetangazwa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Festo Kiswaga, wakati akizungumza na wafanyabiashara mjini Bariadi, Ijumaa Mei 8, 2020.

Kiswaga amewataka wafanyabiashara kuuza sukari kwa bei elekezi ya Sh 2,900 kwa kilo moja na kuweka bayana kuwa operesheni ya kuwasaka wanaokaidi bei hiyo itaanza rasmi Mei 12, 2020.

“Ni dhahiri kwamba asilimia kubwa ya wafanyabiashara wameshindwa kufuata maagizo ya serikali ya kuuza sukari kwa bei ya shilingi 2,900, hivyo kuanzia Jumanne ya tarehe 12 mwezi huu tutafanya operesheni kali kwenye maduka yote na tutakaokuta wamekiuka tutawachukulia hatua za kisheria," amesema Kiswaga na kuelezea kukerwa kwake na upandishaji bei ya sukari kipindi hiki cha mfungo wa Mwenzi Mtukufu wa Ramadhan.

Kwa upande wake, Katibu wa Wafanyabiashara Mkoa wa Simiyu, Zebedayo Kingi, amesema wengi wanatumia gharama kubwa kufikisha bidhaa zao mkoani humo hali inayowalazimu kuuza kwa bei ya juu zaidi ya bei elekezi.

Hata hivyo, Kingi amesema wafanyabiashara wa mkoani humo hawana budi kufuata maelekezo ya serikali kwa kuuza sukari kwa bei elekezi ili kuwezesha wananchi wote kumudu ununuzi wa bidhaa hiyo.

Naye mfanyabiashara, Bahati Ntelemko, amesema tatizo la upandishaji bei ya sukari huenda limetokana na kupungua kwa uzalishaji viwandani, huku akionesha wasiwasi wa hatari ya kukosekana kwa bidhaa hiyo, hasa maeneo ya vijijini.

(Hanari na Anita Balingilaki, Bariadi)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages