NEWS

Wednesday 28 April 2021

CCM yawasimamisha wenyeviti wa mitaa Tarime Mji

 

 Katibu wa CCM Wilaya ya Tarime, Hamis Mkaruka Kura akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo asubuhi

 CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Tarime  kimetangaza kuwasimamisha wenyeviti wa mitaa  kadhaa kutoendelea na wadhifa huo kwa madai ya kufanya uasi. 

 

Katibu wa CCM Wilaya ya Tarime, Hamis Mkaruka Kura ametoa tamko hilo kupitia mkutano na waandishi wa habari ofisini kwake, leo Aprili 28, 2021.

 

Mkaruka amesema waliosimamishwa ni wenyeviti wa mitaa walioshiriki mkutano ulioitwa "umoja wa wenyeviti wa mitaa mji wa Tarime" uliofanyika jana kwenye ukumbi wa hoteli moja mjini Tarime na kudai kuwa  hawako tayari kufanya kazi na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Tarime, Elias Ntiruhungwa. 

 

Katibu huyo amesisitiza kuwa waliohusika katika mkutano huo wameasi taratibu za chama hicho.

 

“Wale wote waliosikika wakizungumza kwenye vyombo vya habari kuanzia leo (Aprili 28, 2021) tunawasimamisha uenyeviti mpaka hapo tutakapowaita kwenye vikao vya maadili na vikao vingine kutoa maamuzi mengineyo,” amesema Mkaruka. 

 

Amesema Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Tarime kinaridhshwa na utendaji kazi wa Mkurugenzi huyo wa Mji wa Tarime na kwamba kama kuna wenyeviti wana jambo dhidi yake walipaswa kufuata utaratibu. 

 

“Huyo Mkurugenzi sisi katusadia sana, anafanya vizuri kazi za umma,” amesisitiza Mkaruka. 

 

Ameongeza kuwa mkutano huo umekiuka taratibu za chama hicho tawala huku akikishutumu kikundi cha wafanyabiashara ambacho amedai kiko nyuma ya sakata hilo kwa maslahi binasfi ambayo yanawezea kufifisha utendaji na ufanisi katika Halmashauri  ya Mji wa Tarime. 

 

“Kwanza hatuna kitu kinaitwa umoja wa wenyeviti wa mitaa kisheria na hatuna mwenyekiti wa umoja wa wenyeviti, huo ni uasi,“ amesema Katibu huyo wa CCM. 

 

Mkaruka amesema vikao vyote vinavyojadili maslahi ya Chama vinafanyika ndani ya ukumbi wa CCM Wilaya, hivyo chama hicho kinaamini kilichofanywa na wenyeviti hao sio sahihi. 

 

“Na ukumbi wamekodi na wakanywa na soda, ni nani aliwafadhili, na tuna ukumbi wa kutosha watu 600 na hakuna mtu aliomba akanyimwa, tafasiri yake tunajua kuna watu wako nyuma yao ambao ni waasi wenzao na tunaendelea kutafuta mmoja mmoja,(akimanisha waliowezesha mkutano huo kufanyika),”  amesema Mkaruka bila kuweka wazi idadi wa wenyeviti wa mitaa waliosimamishwa wadhfa wao. 

 

Katika hatua nyingine, Katibu huyo wa CCM Wilaya ameomba mamlaka husika kutatua mgogoro wa vibanda vya wafanyabiashara  katika mji huo badala ya kuingia katika mabishano. 

 

“Chama Cha Mapinduzi tunatoa agizo leo, ndani ya siku saba tupate majibu, tofauti na hapo tutachukua hatua kwa kila mhusika,“ ametahadharisha Mkaruka.

 

(Habari na picha: Mara Online News)

 


No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages