NEWS

Thursday 20 May 2021

Tarime Mji kuanza ujenzi wa soko la kisasa



Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Tarime, Daniel Komote (aliyesimama) akizungumza katika kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo, leo.

  

SERIKALI imeiruhusu Halmashauri ya Mji wa Tarime mkoani Mara kutumia Shilingi bilioni tatu kugharimia ujenzi wa soko la kisasa la mji huo kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 utakaoanza Julai mwaka huu wa 2021. Bajeti ya ujenzi huo ni Shilingi bilioni nane.

Hayo yamebainika kwenye kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika leo Mei 20, 2021 kwenye ukumbi wa Shule ya Sekondari ya Tarime, cha kupokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika kata mbalimbali zinazounda halmashauri hiyo.

Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Daniel Komote ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Nkende, amesema ujenzi wa soko hilo ulisitishwa na Serikali tangu mwaka juzi, hivyo kusababisha usumbufu mkubwa kwa wafanyabiashara.


Hawa ndio madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Tarime.

“Waheshimiwa madiwani napenda kuwajulisha kuwa ujenzi wa soko letu ambao ulisitishwa kwa barua na Serikali Kuu tangu mwaka 2019, utaanza mwaka mpya wa fedha 2021/2022 baada ya kuonekana tumekidhi vigezo,” amesema Komote ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Serikali za Mitaa Tanzania (ALAT) Mkoa wa Mara.

Hata hivyo, Komote amesema itabidi wakae tena na mshauri wa ujenzi wajadiliane namna ya kupunguza gharama za ujenzi kwani bei ya ujenzi huo itakuwa imepanda kutokana na vifaa vya ujenzi kupanda gharama tangu tenda ilipotangazwa awali, ambapo wakati huo ujenzi ungeghalimu Shilingi bilioni nane.

Pia, Komote ameomba Serikali kuwaongezea watendaji wa mitaa kwani halmashauri hiyo yenye mitaa 81 ina watendaji 15, hali ambayo imelalalamikiwa na madiwani akiwemo wa Kata ya Sabasaba, Raymond Mwema aliyesema kata yake yenye mitaa 12 haina mtendaji.

(Habari na picha: Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages