NEWS

Tuesday 6 July 2021

Benki ya Dunia kuing'arisha Tarime Mji kwa barabara, stendi za mabasi




HALMASHAURI ya Mji wa Tarime mkoani Mara, imefanikiwa kuingia kwenye orodha ya miji 45 ambayo hunufaika na miradi inayofadhiliwa na Benki ya Dunia (WB), kupitia mpango wake wa kuzijengea uwezo halmashauri za miji (TACTIC) ili kupanua vyanzo vya mapato.

Akizungumza na wadau mbalimbali wa maendeleo leo Julai 6, 2021, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji huo, Elias Ntiruhungwa amesema wamefanikiwa kukidhi vigezo na kupata miradi minne muhimu.

“Baada ya halmshauri yetu kufanikiwa kuingia kwenye mpango wa TACTIC, tumepatiwa mradi wa kujengewa barabara yenye urefu wa kilomita 18, ujenzi wa kituo cha mabasi Kemange, kukarabati stendi ya mabasi ya zamani, kujengewa dampo la kisasa Magena na kununuliwa magari ya kusomba taka,” amesema Ntiruhungwa.


Mkurugenzi Ntiruhungwa akizungumza katika mkutano huo

Ntituhungwa ameafanua kuwa miradi ya barabara hizo ambazo zinazunguka mji wa Tarime, zitajengwa kwa kiwango cha lami na kuwekewa taa na alama za barabarani, stendi ya mabasi itakuwa bora yenye vibanda 220 vya maduka, sehemu za kupumzikia abiria na maeneo ya maegesho ya magari na pikipiki.

Wakichangia maoni katika mkutano huo, baadhi ya wadau wameomba hizo barabara ziwekewe majina kwenye vibao haraka ili zijulikane kuepuka ‘kuchakachuliwa’ na wengine wameshauri bajeti ya halmashauri iliyokuwa umetengwa kutekeleza miradi hiyo, ielekezwe kwenye barabara za kuelekea vijijini.



Baadhi ya barabara hizo zimetajwa majina yake kuwa ni ile ya Market Rosoti, Amazoni, Freezone, Biafra, A.M.A Hotel, Turwa Empire, Machinjioni, Posta A na Sabasaba SDA.

Pia wadau wameshauri kwamba baada ya halmshauri hiyo kupewa msaada huo, sasa ielekeze nguvu kwenye barabara za Kenyamanyori, Nyandoto na Korotambe ambazo ni muhimu kwa wakulima.



(Imeandikwa na Mobini Sarya)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages