NEWS

Sunday 8 August 2021

JATU yatoa mrejesho kwa wakulima, yawashukuru wadau waliopaisha mauzo ya hisa zake




KAMPUNI ya JATU (JATU PLC) imezishukuru taasisi na wadau wote waliohusika katika mchakato wa kuwezesha mauzo ya hisa zake kwa umma.

Mkurugenzi Mkuu (DG) wa JATU PCL, Peter Isare Gasaya ametaja taasisi na wadau hao kuwa ni pamoja na Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) na Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE).


DG wa JATU PCL, Peter Isare Gasaya.

DG Gasaya ametaja nyingine kuwa ni Kampuni ya Archco Limited (Mshauri Mteule), Kampuni ya Mafuru & Co. Advocates (Mshauri wa Sheria) na Kampuni ya Diamond Finacial Services (Wakaguzi wa Hesabu).

“Aidha, tunapenda kutoa shukrani na pongezi za dhati kwa wawekezaji wapya na wadau wote, kwa ushirikiano na imani waliyonayo kwa kampuni ya JATU PLC,” ameongeza.


Wanachama na wawekezaji wa JATU PLC wakimsikiliza DG Gasaya katika mkutano huo

DG Gasaya ametoa pongezi hizo jana Agosti 7, 2021 jijini Dar es Salaam, wakati akitoa mrejesho katika mkutano mkuu wa wakulima wa JATU PLC, waliolima mpunga na mahindi msimu uliopita wa 2020-2021.
 
Leo Agosti 8, kampuni hiyo itatoa mrejesho huo kwa wanachama na wawekezaji wake waliopo Kanda ya Ziwa, katika mkutano utakaofanyika jijini Mwanza.
 
Oktoba 2021, kampuni hiyo itatoa mrejesho wa mazao ya maharage na alizeti.

Kwa mujibu wa DG Gasaya, mauzo ya hisa za JATU PLC kwa umma yamefanyika kwa mafanikio, ambapo imeuza hisa 15,526,372 sawa na asilimia 104 na kuvuka lengo la kuuza hisa 15,000,000.


Wafanyakazi wa JATU PCL kitengo cha mauzo wakimsikiliza na kumhudumia mteja

Mei 31, 2021, CMSA iliidhinisha maombi ya JATU PLC kuuza hisa 15,000,000 kwa umma kwenye soko la awali, zenye thamani ya Sh bilioni 7.5, kwa bei ya Sh 500 kwa kila hisa, ambapo mauzo ya hisa yalifunguliwa Juni 1, 2021 na kufungwa Julai 15, 2021.

(Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages