NEWS

Tuesday 7 September 2021

Makuruma awapa somo watendaji, madiwani Serengeti




MAOFISA watendaji na madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti mkoani Mara, wamehimizwa kuchapa kazi na kushirikiana katika utumishi wa umma, kwa ustawi wa maendeleo ya halmashauri hiyo.

“Kila mmoja kwa nafasi yake afanye kazi kwa bidii na weledi, ili halmashauri yetu iende vizuri hata katika ukusanyaji mapato na utekelezaji miradi ya maendeleo,” Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Ayub Mwita Makuruma amesisitiza.

Makuruma ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Busawe kwa tiketi ya CCM, ameyasema hayo wakati akifungua kikao cha baraza la madiwani mjini Mugumu leo Septemba 7, 2021.


Makuruma akifungua kikao hicho

Amesema ushirikiano hafifu wa maofisa watendaji na madiwani unachangia miradi ya huduma za kijamii kutekelezwa chini ya kiwango.

“Hatutawavumilia watendaji na madiwani watakaoonesha kutotoa ushirikiano. Halmashauri ni ya madiwani na watendaji,” Makuruma ameongeza.

Madiwani kikaoni

Mwenyekiti huyo ametumia nafasi hiyo pia kumpongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri (DED) hiyo, Kivuma Hamisi Msangi, kwa kuchukua hatua za kuboresha uwajibikaji wa watumishi kwa wananchi.

Akizungumza katika kikao hicho, DED Msangi ameahidi kuimarisha usimamizi kwa watumishi walio chini yake na ushirikiano kwa madiwani.

“Ofisi yangu itasimamia vizuri watumishi na kuwapa madiwani ushirikiano wa dhati, ili kuchochea maendeleo ya halmashauri yetu,” DED Msangi amesisitiza.


DED Msangi akizungumza kikaoni

Kikao hicho cha madiwani kitaendeleo kesho, baada ya kupokea taarifa za maendeleo kutoka kata zote 30 zinazounda halmashauri hiyo leo.

(Habari na picha zote: Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages