NEWS

Wednesday 13 October 2021

Wasimamizi wa ukusanyaji mapato Serengeti matatani, madiwani wapitisha azimio la kuwatumbua




BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti mkoani Mara, limepitisha azimio la kutengua uteuzi wa wasimamizi wote wa ukusanyaji mapato katika vyanzo vya ndani, kutokana na tuhuma za hujuma na wizi.

Kaimu Mkurugenzi Mtendji wa Halmashauri hiyo, Wambura Sunday ameahidi kutekeleza azimio hilo haraka iwezekanavyo.

“Tutaondoa wasimamizi wote wa ukusanyaji mapato. Tutabadilisha na kuongeza usimamizi na ufuatiliani,” Sunday amekiahidi kikao cha baraza la madiwani mjini Mugumu, wiki iliyopita.

Hatua hiyo inayolenga kudhibiti upotevu wa mapato na kuongeza ufanisi katika ukusanyaji, ni zao la msukumo wa madiwani wa halmashauri hiyo waliotilia shaka uaminifu wa wasimamizi hao.

“Lazima tupate watu waaminifu, na wasio waaminifu lazima wachukuliwe hatua,” Diwani wa Kata ya Natta, Juma Porini amesisitiza.


Ayubu Mwita Makuruma

Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Ayubu Mwita Makuruma amekazia hoja hiyo akisema “Tumegundua mifumo ya ukusanyaji wa mapato iliyopo sio mizuri, watendaji wengi siyo waaminifu, waondolewe wote na tupate sura mpya.”

Ameongeza “Lakini katika usimamizi huo, sasa tumekubaliana kwamba madiwani wahusike katika kufuatilia [ukusanyaji mapato] kwa kushirikiana na wataalamu.”

(Na Mwandishi wa Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages