NEWS

Sunday 26 December 2021

Ukoo wa Chifu Burito Nyerere wakutana kuweka mikakati kabambe



UKOO wa Chifu Nyerere Burito ambao ni chimbuko la Baba wa Taifa la Tanzania, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, umekutana kwa ajili ya kujitathmini na kuweka mikakati ya maendeleo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Chini ya uongozi wa Mkuu wa Ukoo huo, Chifu Japhet, mkutano huo umefanyika jana Desemba 26, 2021 katika kijiji cha Butiama mkoani Mara, ukihusisha wanaukoo wasiopungua 120.



Pamoja na masuala mengine ya kiukoo, wamedhamiria kufanya maadhimisho ya Miaka 100 ya Kuzaliwa kwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, 13 Aprili 2022.

Imeelezwa na Chifu Wanzagi kuwa waasisi wa Ukoo huo waliweka misingi ya kukutana kila mwisho wa mwaka, hivyo na wao hawana budi kuizingatia na kuirithisha kwa vizazi vyao vya sasa na vijavyo.



“Huu ni ukoo wenye asili ya uongozi, ni Machifu wa Wazanaki, lakini pia ni chimbuko la mtu aliyeongoza Taifa la Tanganyika kupata Uhuru,” Chifu Wanzagi amesema na kuendelea:

“Hata baada ya kifo, Kanisa Katoliki linaendelea na mchakato wa kumtangaza kuwa Mwenye Heri na baadaye kwa uweza wa Mwenyezi Mungu atatangazwa kuwa Mtakatifu, kwa hali hiyo hatuwezi kuacha kuzingatia misingi ya maadili tuliyokuzwa nayo.”



Mchakato wa mtu kutangazwa kuwa Mtakatifu katika baadhi ya mambo huhusisha familia na ukoo wake, hivyo Chifu Wanzagi amesema wanaukoo huo hawatakiwi kuwa kikwazo.

Mkutano huo umehudhuriwa na viongozi wa kiserikali na kisiasa, wakiwemo Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Butiama, Yohana Mirumbe na Mkuu wa Wilaya hiyo, Moses Kaegele ambaye ametunukiwa uzawa wa ukoo huo.



Mkutano huo umekubaliana kumtunuku jina la Magembe Nyakusamaga, ambaye hitoria inasema alikuwa mdogo wake Chifu Nyerere Burito ambaye ni baba mzazi wa Mwalimu Nyerere.

Naye Kaegele amepokea heshima hiyo akiahidi kushirikiana na ukoo huo katika kila jambo kwa kadiri atakavyoshirikishwa.

(Habari na picha zote: Sauti ya Mara)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages