NEWS

Friday 27 May 2022

Wadau wahamasishwa kujivunia na kutangaza kahawa inayozalishwa kanda ya Mara



WADAU wamehamasishwa kuitangaza zaidi kahawa inayolimwa kanda ya Mara, kwa kuboresha kilimo cha zao hilo la biashara.

Changamoto hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya (DC) ya Rorya, Juma Chikoka, wakati akifungua mkutano wa wadau wa kahawa kanda ya Mara katika ukumbi wa Kanisa Katoliki mjini Tarime, leo Mei 27, 2022.



DC Chikoka amesema kahawa aina ya Arabica inaliyozalishwa katika wilaya ya Tarime mkoani Mara inasifika kwa ubora, hivyo wakulima wanapaswa kutumia fursa hiyo kuboresha kilimo na uzalishaji wa zao hilo.

“Sisi viongozi tutakuwa mfano bora namba moja katika kilimo cha kahawa,” amesema Chikoka na kuongeza kuwa dhamira ya Serikali ni kuona kilimo cha zao hilo kinafanyika kibiashara na kwa tija, ili kuinua uchumi wa wakulima na taifa kwa ujumla.



“Kilimo cha kahawa chenye tija kitapunguza umaskini na kuongeza mzunguko wa fedha kwa wananchi,” amesema DC Chikoka.

Naye Meneja wa idara ya maendeleo ya zao hilo kutoka Bodi ya Kahawa Tanzania, Edmond Zani amesema kahawa ni miongoni mwa mazao saba ya kimkakati yaliyoidhinishwa na Serikali nchini, na kwamba hadi sasa kilimo hicho kinanufaisha watu zaidi ya milioni 2.4 nchini.



“Umuhimu wa zao la kahawa unatokana na mchango wake katika kipato cha mtu mmoja mmoja, mapato ya halmashauri za wilaya, chanzo cha fedha za kigeni na katika ujenzi wa sekta ya viwanda,” amesema Zani.

Ametaja changamoto zilizopo kuwa ni pamoja na tija ndogo inayosababisha mapato kidogo, matumizi duni ya mbolea za viwandani, upungufu wa huduma za ugani, mabadiliko ya tabianchi na kutozingatia kanuni za kilimo bora.

Hata hivyo, Zani amesema Bodi ya Kahawa ina mkakati wa kuanzisha mashamba ya pamoja (block farm), unaolenga kuboresha kilimo na kuongeza uzalishaji wa zao hilo katika wilaya mbalimbali.

(Habari na picha zote: Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages