NEWS

Saturday 26 November 2022

Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia: Barrick wazindua kampeni ya elimu kwa vijiji 11 North Mara



Na Mara Online News
---------------------------------

KAMPUNI ya Barrick imeongeza nguvu kwenye kampeni ya kupinga ukatili wa kijinisa katika vijiji 11 vinavyozunguka Mgodi wa Dhahabu wa North Mara.

Barrick imezindua kampeni hiyo Ijumaa Novemba 25, 2022 katika hafla iliyofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari Ingwe iliyopo kilomita chache kutoka mgodi huo.

Mmoja wa wanasheria kutoka TAWLA akielezea madhara ya ukatili wa kijinisai na jinsi ya kujikinga kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari JK Nyerere iliyopo kijiji cha Nyamwaga, kilomita chache kutoka Mgodi wa Dhahabu wa North Mara, leo. (Picha na Mara Online News)

Kampeni hiyo ambayo Baarrick imeiandaa kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Tarime (Vijijini), ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia inaweza kusaidia kuokoa mamia ya wasichana walio kwenye hatari ya kufanyiwa ukeketaji mwezi ujayo.

Barrick North Mara inashirikisha timu ya wanasheria kutoka Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA), maofisa ustawi wa jamii kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Tarime (Vijjini), dawati la jinsia Polisi, viongozi wa dini, wenyeviti na watendji wa vijiji kutoa elimu ya masuala mbalimbali ya kisheria ili kukabili vitendo vya ukatili wa kijinsia katika vijiji hivyo 11.

“Tumezindua kampeni ya kupinga ukatili wa kijinsia ambapo tutafikia vijiji 11 vinazunguka mgodi wa Barrick North Mara,” Afisa Mahusiano wa mgodi huo, Zachayo Makobero amesema wakati wa kampeni hiyo leo Jumamosi Novemba 26, 2022 katika Shule ya Sekondari JK Nyerere iliyopo Nyamwaga.

Makobero akizungumza na wanafunzi wa Sekondari ya JK Nyerere wakati wa kampeni hiyo

Kwa sasa Mgodi wa Dhahabu wa North Mara unaendeshwa na Barrick kwa ubia na Serikali ya Tanzania kupitia kampuni ya Twiga Minerals.

Vijiji vilivyo jirani na mgodi huo ambavyo vinafikiwa na kampeni hiyo ni Nyangoto, Kewanja, Mjini Kati, Matongo, Kerende, Nyabichune, Genkuru, Msege, Komarera, Nyakunguru na Nyamwaga.

“Tunawafikia pia viongozi wa dini, wanafunzi wa kike na wananchi kwa ujumla kwenye mikutano ya hadhara na majumba ya ibada,” Makobero amesema na kuendelea:

“Lengo kuu la kampeni hii ni kutoa elimu ya kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia katika vijiji hivi ukiwemo ukeketaji, lakini pia elimu ya masuala mbalimbali ya kisheria kama vile ardhi na mirathi.”


Kaulimbiu ya kampemi hiyo inasema: “Kataa Ukatili wa Kijinsia - Say no to Gender Based Violence”.

Kampeni hiyo imefanyika kipindi hiki cha kuelekea msimu wa tohara inayohusisha ukeketji watoto wa kike katika baadhi ya maeneo wilayani Tarime.

Kwa mujibu wa sheria, ukeketaji ni kosa la jinai. Lakini bado baadhi ya jamii zinaendelea kukumbatia mila hiyo ambayo inaripotiwa kuendelea kuuumiza mamia ya watoto wa kike kwa namna mabalimbali, ikiwemo kuchangia kukatisha ndoto zao za elimu.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages