NEWS

Monday 9 January 2023

Waitara: Tumeandika historia Tarime Vijijini keki ya CSR Barrick North Mara



Na Mwandishi Wetu, Tarime
-------------------------------------------

MBUNGE wa Jimbo la Tarime Vijijini, Mwita Waitara, amesema uongozi wake umeandika historia nzuri, baada ya kuwezesha kila kijiji kunufaika na uwepo wa Mgodi wa Dhahabu wa North Mara katika jimbo hilo lenye utajiri mkubwa wa madini.

Mgodi huo unaendeshwa na kampuni ya uchimbaji madini ya Barrick, kwa ubia na Serikali ya Tanzania kupitia Kampuni ya Twiga Minerals.

Kampuni ya Barrick imekuwa ikitenga mabilioni ya fedha kwa ajili ya kugharimia miradi ya kijamii kupitia mpango wake wa Uwajibikaji kwa Uhuduma za Jamii (CSR) katika vijiji 11 vilivyo jirani na mgodi wa North Mara tangu mwaka 2019.

Lakini kwa mara ya kwanza, kuanzia mwaka 2022 viijiji 77 vilivyokuwa vinaachwa kando vimepewa asilimia 30 ya ‘keki’ hiyo, huku asilimia 70 ikibaki kwenye vijiji 11, jambo ambalo Mbunge Waitara analiona kama moja ya mafanikio makubwa ambayo jimbo hilo limepata katika kipindi cha uongozi wake.

Kwa mujibu wa Mbunge Waitara, mwaka jana Halmashauri ya Wilaya ya Tarime (Vijijini) imegawa kwenye shilingi bilioni 5.7 ilizopata kutoka CRS Barrick North Mara na kwamba mwaka huu itapewa bilioni 5.7 nyingine kwa ajili ya kugharimia utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

“Kwenye uongozi wetu tumefanya jambo kubwa. Fedha ya CSR ilikuwa inaenda kweye kata tano zenye vijiji 11, lakini kipindi hiki tumepeleka fedha za CSR kwenye kata zote 26 zenye vijjiji 88,” Waitara alisema wakati wa ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo katika kata mbalimbali jimboni kwake, hivi karibuni.

Akiwa katani Komaswa, Mbunge huyo anyetokana na Chama Cha Mapinduzi (CCM), alishuduia maendeleo ya miradi mbalimbali ya CSR, ukiwemo ujenzi wa bafu 11 na ununuzi wa vitanda 70 katika Shule ya Sekondari Manga yenye wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha sita.

Alisema kila kijiji cha Halmashauri ya Tarime ya Tarime (Vijijini) kinashuhudia mageuzi makubwa ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo hayajawahi kushuhudiwa tangu Tanzania ipate uhuru, kutokana na fedha zinazotolewa na Serikali na Kampuni ya Barrick kupitia mpango wake wa CSR.

“Ukipanga ratiba ya kutembelea jimbo letu la Tarime Vijijini utakuta miradi mbalimbali ya maendeeleo inatekelezwa katika kila kijiji. Jambo la muhimu ni wananchi kuendelea kutoa ushirikiano na usimamazi mzuri,” alisema Mbunge Waitara ambaye amewahi kuhudumu kama Naibu Waziri katika wizara mbalimbali miaka ya hivi karibuni.

Mbunge Mwita Waitara

Taarifa zilizopo zinaonesha kuwa Kampuni ya Barrick ilianza kutenga mabilioni ya fedha kwa ajili ya kugharimia utekelezaji wa miradi ya huduma za kijamii katika vijiji 11 vinavyozunguka mgodi wa North Mara mwaka 2019, ambapo kwa mara ya kwanza kupitia mpango wake w CSR ilitenga Dola za Kimarekani milioni 2.5.

Aidha, kampuni hiyo ilitenga Dola milioni 1.8 kwa ajili ya kugharimia miradi ya CSR kwa mwaka 2020, Dola milioni 1.8 pia kwa mwaka 2021 na Dola milioni 1.18 kwa mwaka jana (2022).

Miezi michache iliyopita, shilingi bilioni 7.714 kutoka CSR Barrick North Mara zilipata baraka zote kwa ajili ya kugharimia utekelezaji wa miradi ya kijamii katika halmashauri hiyo ya Tarime Vijijini.

Waitara alisema usimamizi mzuri wa utekelezaji wa miradi inayogharimiwa na fedha za Serikali na CSR kutoka Kampuni ya Barrick utaleta mageuzi makubwa katika sekta mbalimbali kama vile elimu, afya na maji ndani ya jimbo hilo.

Katika hatua nyingine, Mbunge Waitara alikagua ujenzi wa kituo kipya cha afya katika kata ya Kwihanja ambacho ujenzi wake unaripotiwa kwenda kwa kasi, baada ya Serikali kutoa shilingi milioni 500 kugharimia utekelezaji wa mradi huo.

Kiongoi huyo wa wananchi alisifu utaratibu wa sasa wa Serikali ya Awamu ya Sita wa kutoa fedha za kugharimia miradi ya maendeleo kabla ya shughuli husika kuanza.

Chanzo: SAUTI YA MARA

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages