NEWS

Monday 30 October 2023

TEA yakamilisha ujenzi wa vyumba vitatu vya madarasa katani Nyanungu kwa ufadhili wa TANAPA



Muonekano wa mbele wa vyumba vitatu vya madarasa vilivyojengwa na TEA katika Shule ya Msingi Kegonga katika kata ya Nyanungu wilayani Tarime, kwa ufadhili wa TANAPA. (Picha na Sauti ya Mara)
-------------------------------------------

NA MWANDISHI MAALUMU
------------------------------------------ 

MAMLAKA ya Elimu Tanzania (TEA) imekalimisha ujenzi wa vyumba vitatu vya madarasa ya kisasa katika Shule ya Msingi Kegonga iliyopo kata ya Nyanungu, wilaya ya Tarime, mkoani Mara. 

Taarifa zilizopo zinaonesha kuwa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) ndilo lilitoa shilingi zaidi ya milioni 70 kwa ajili ya kugharimia ujenzi wa madarasa hayo - kupitia mpango wake wa ujirani mwema. 

Kegonga ni kimojawapo cha vijiji vya Halmashauri ya Wilaya ya Tarime (Vijijini) vinavyopakana na Hifadhi ya Taifa Serengeti. 

“Madarasa yote matatu yamekamilika hadi vigai, na sasa tunasubiri kukabidhiwa rasmi,” Mwenyekiti wa Serekali ya Kijiji cha Kegonga, Waryoba Mwita Mogoyo aliiambia Sauti ya Mara. 

Sauti ya Mara ilitembelea shule hiyo wiki iliyopita na kushuhudia vyumba hivyo vitatu vikiwa vimekamilika. 

Kwa mujibu wa Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Kegonga, Moses Michael Mwakalakwala, kukamilika kwa vyumba hivyo kutasaidia kupunguza msongamano wa wanafunzi katika shule hiyo, ambayo kwa sasa ina wanafunzi zaidi ya 1,200. 

“Tunashukuru sana TANAPA kwa kutujengea haya madarasa, tunaomba waendelee kutasaidia,” alisema Mwl Mkwalakwala. 

Wanavijiji wanasema madarasa hayo yamejengwa kwa viwango bora na kwamba yameifanya shule hiyo kongwe kuwa na sura mpya ya kisasa. 

Chanzo: Gazeti la SAUTI YA MARA
#Tunakuhabarisha Ukweli kwa Weledi

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages