NEWS

Friday 8 December 2023

Kuelekea uzinduzi wa Tarime Runners Club: Timu yapeleka msaada wa vifaa vya usafi wodi za mama na mtoto



Msaada wa madumu ya kuhifadhi taka yaliyotolewa na Tarime Runners Club kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime, leo Desemba 8, 2023.
----------------------------------------------------

Na Mwandishi wa Mara
Online News, Tarime
-------------------------------

Timu ya Tarime Runners Club imeshiriki usafi na kuipatia Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime msaada wa vifaa vya usafi, leo Desemba 8, 2023. 

Imefanya usafi, hususan wa kufyeka nyasi na kukabidhi msaada wa sabuni za unga na madumu ya kuhifadhi taka ili kutunza mazingira, vyote vikielekezwa kwenye wodi za mama na watoto. 

Afisa Mahusiano wa Tarime Runners Club, Mwl Chacha Heche amesema wameyafanya hayo kuhamasisha usafi wa mazingira hospitalini hapo kipindi hiki cha kuelekea uzinduzi wa klabu hiyo utakaofanyika Desemba 16, 2023.


Wakifanya usafi

“Tumekuja kumuunga mkono Mkurugenzi [wa Tarime Mji] kwa kutoa msaada wa sabuni na madumu ya kuhifadhi uchafu katika wodi hizi ili kutunza mazingira. 

“Tumefanya usafi kwa mikono yetu kuhamasisha usafi… watumishi wanapofanya usafi isionekane kama wanashurutishwa… wao hufanya kazi tukiwa tumelala tunashindwa kuwapa ushirikiano,” amesema Mwl Chacha. 


Timu ya Tarime Runners Clab ikifurahia kupiga picha ya pamoja ilipokwenda kufanya usafi na kuipatia Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime msaada wa vifaa vya usafi.
--------------------------------------------------

Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dkt Yonamu Charles ameishukuru Klabu hiyo na kuiomba iendelee kuwatembelea kila inapopata nafasi. 

“Tunathamini sana mchango wenu wa kuthamini hospitali na jamii tunayoihudumia hapa, hizi dust bins (madumu ya kuhifadhi taka) zitatusaidia kutunza mazingira kwa kuyaweka safi, mbarikiwe sana, mkipata nafasi msichoke kuja tena,” amesema Dkt Yonamu.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages