NEWS

Tuesday 16 January 2024

Nyambari Nyangwine ampongeza Dkt Nchimbi, asema CCM imefanya chaguo sahihi, ampa tano Rais Samia



Balozi Dkt Emmanuel John Nchimbi
-------------------------------------------------

Na Mwandishi Wetu

-----------------------------


ALIYEWAHI kuwa Mbunge wa Jimbo la Tarime mkoani Mara, Nyambari Nyangwine (CCM), amempongeza Balozi Dkt Emmanuel John Nchimbi kwa kuaminiwa na kuteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa chama tawala - CCM.

“Kwa kifupi, nimepokea taarifa za uteuzi huo wa Dkt Nchimbi kwa furaha sana, na nitumie nafasi hii kumpongeza sana,” amesema Nyangwine katika mazungumzo na Mara Online News kwa njia ya simu mapema leo.

Ameongeza: “Hakika Chama kimepata mtu sahihi, Dkt Nchimbi ni msikivu, hana papara, ni mtu anayeweka fikra kwenye mizani kwanza kabla ya kutoa maamuzi, na maamuzi yake yanakuwa na maslahi mapana kwa Watanzania.”

Nyambari Nyangwine
------------------------------
Nyambari ametumia nafasi hiyo pia kumpongeza Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuongoza vizuri vikao vilivyofanikisha uteuzi wa Balozi Dkt Nchimbi. “Ninampongeza sana na Mwenyekiti wetu wa CCM Taifa, Mheshimiwa Rais Dkt Samia kwa kazi kubwa na nzuri,” amesema.

Jana Jumatatu, Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, ilipokea na kuidhinisha pendekezo la Kamati Kuu (CC) ya Chama hicho - la kumteua Balozi Dkt Emmanuel John Nchimbi kuwa Katibu Mkuu wa CCM.


Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Dkt Samia akisalimiana na Katibu Mkuu mpya wa Chama hicho tawala, Balozi Dkt Nchimbi, jana mara baada ya uteuzi wake mjini Unguja, Zanzibar,.
------------------------------------------------
NEC ya CCM ilipitisha uteuzi huo wa Balozi Dkt Nchimbi kwenye kikao chake maalum, kilichofanyika Januari 15, 2024 mjini Unguja, Zanzibar.

Balozi Dkt Nchimbi anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Daniel Chongolo aliyejiuzulu Novemba 2023.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages