NEWS

Thursday 7 March 2024

Prof Muhongo alivyong’ara ziara ya Waziri Mkuu Majaliwa mkoani Mara, Serikali yamhakikishia majisafi, ujenzi wa barabara za lami Musoma Vijijini



Mbunge wa Musoma Vijijini, Prof Sospeter Muhongo (kulia) akimkabidhi Waziri Mkuu Kassim Majaliwa nakala za vitabu vya utekelezaji wa Ilani ya CCM jimboni humo, wiki iliyopita.
----------------------------------------

Na MWANDISHI WETU, Musoma
--------------------------------------------------


WAZILI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa amempongeza Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini, Prof Sospeter Muhongo, akisema hata Rais Dkt Samia Suhuhu Hassana anampenda kutokana na juhudi kubwa anazofanya kuwaletea wananchi wake maendeleo.

Majaliwa alitoa kauli hiyo wakati wa ziara yake Musoma Vijijini wiki iliyopita na kuwataka wananchi wa jimbo hilo kumkubatia azidi kuwaletea maendeleo ya kisekta.

“Profesa huyu [Muhongo] msije mkampoteza, huyu profesa huyu, kwanza ana heshima serikalini, Rais anamjua vizuri na anampenda sana kwa sababu ni kiongozi mahiri,” alisisitiza Waziri Mkuu Majaliwa.

Akizungumzia ombi la maji ya bomba kwa ajili ya wananchi wa maeneo ya Kiriba Musoma Vijijini, Mtendaji Mkuu huyo wa Serikali alisema wana haki ya kuunganishiwa huduma hiyo kwani bomba kuu la maji yanayopelekwa jimbo jirani la Butiama linapita hapo.

“Hatutoi maji hapa tukayapeleka Butiama bila huku kuwa na maji, ni lazima maji hayo yasambae kwenye vijiji vyote humu na kuongeza miradi mingine ili kila kijiji kiwe na maji ya kutosha. Kazi hii ni endelevu na ndiyo maagizo ya Rais wetu,” alisema na kuwahakikishia wananchi hao kuwa Serikali itateendelea kuwahudumia miradi ya kijamii ili kukidhi mahitaji yao.

Awali, Profesa Muhongo aliwasilisha kwa Waziri Mkuu changamoto ya maji ya bomba katika maeneo ya Kiriba akisema wananchi hawajawahi kupata huduma hiyo licha ya kuishi Jirani na Ziwa Victoria.

Kwa upande wake Waziri wa Maji, Jumaa Aweso aliwatoa hofu wananchi wa maeneo hayo kwa kuwaahidi kuunganishiwa huduma hiyo siku chache zijazo.

“Mheshimiwa Waziri Mkuu, mimi Waziri wa Maji, kwa wana-Kiriba kupata majisafi naendea kutekeleza. Wahandisi wa maji tunatambua mnapojenga mradi mkubwa bomba kuu linapopita katika kijiji upande wa kulia na kushoto wananchi wa vijiji vile lazima wapate huduma ya majisafi na salama.

“Kwa hiyo maelekezo ambayo nimeyatoa kazi ya kuyatoa maji katika bomba kuu na kuyaleta hapa Kiriba ianze mara moja ili wananchi hawa waweze kupata huduma ya majisafi na salama,” aliagiza Waziri Aweso.

Aidha, Serikali imeahidi kuendelea kujenga kwa kiwango cha lami barabara la Musoma-Makojo-Busekera yenye urefu wa kilomita 92.

Waziri Mkuu Majaliwa Majaliwa liwaeleza wana-Musoma Vijijini kuhusu uamuzi wa Serikali kuendelea kutoa fedha nyingi za utekelezaji wa miradi ya maendeleo vijijini kwao.

Alisema Serikali itaendelea kujenga barabara yao kuu na muhimu ya Musoma-Makojo-Busekera ambayo tayari kilomita tano zimeishawekewa lami, na imo kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Godfrey Kasekenya alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Samia imeshaidhinisha ujenzi wake.

“Tunategemea Mheshimiwa Waziri Mkuu muda wowote barabara hii itatangazwa kwa sababu Mheshimiwa Rais ameshatoa kibali tuanze kuijenga yote tukianza na kilomita 40,” alisema Kasekenya.

Katika hatua nyingine, Prof Muhongo alijivunia mbele ya Waziri Mkuu Majaliwa utekelezaji wa Ilani ya chama tawala - CCM akisema Musoma Vijijini ni miongoni mwa majimbo machache nchini yanayoongoza kwa kuitekeleza kwa vitendo.

“Waziri Mkuu katika utekelezaji wa Ilani, sisi Musoma Vijijini jimbo letu na ninaweza kusema kwa kujiami kabisa ni katika majimbo bora tatu ndani ya nchi yetu kwenye utekelezaji wa Ilani ya CCM, na hii ni kwa sababu sisi tunajiongeza.

“Serikali Kuu inatuparia fedha, hawa wananchi huku kwetu wanachangia nguvu kazi, wanachangia fedha zao, mbunge anachangia, madiwani wanachangia, viongozi wa serikali za vijiji wanachangia, ndiyo maana kwa miaka miwili tumeweza kujenga madaraja zaidi ya 600,” alisema Prof Muhongo.

Prof Muhongo aliendelea: “Wana-Musoma Vijijini tunaendelea kuishukuru Serikali yetu chini ya uongozi mzuri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha nyingi za kufadhili miradi ya maendeleo katika vijijini vyetu.

“Tunamshukuru sana Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa kututembelea jimboni mwetu, na kwa kuendelea kufuatilia utekelezaji wa miradi yetu ya maendeleo ambayo ni kielelezo cha mafanikio ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya Mwaka 2020-2025.”

Katika ziara yake hiyo ya Musoma Vijijini, Waziri Mkuu Majaliwa pia aliweka jiwe la msingi katika jengo la utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Musoma.
Chanzo: Gazeti la SAUTI YA MARA
#Ukweli kwa Weledi

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages