NEWS

Monday 1 July 2024

Mfanyabiashara maarufu Yusuf Manji afariki dunia Marekani



Yusuf Manji enzi ya uhai
---------------------------------

Mfanyabiashara maarufu nchini Tanzania, Mwenyekiti na mdhamini wa zamani wa Yanga SC, Yusuf Manji amefariki Dunia akiwa na umri wa miaka 59.

Jana, mtoto wake, Mehboub Manji alithibitisha kifo cha baba yake huyo aliyekuwa Mkurugenzi wa Kampuni ya Quality Group Limited, akisema alifariki dunia Jumamosi Juni 29, 2024 saa 6:00 usiku katika jimbo la Florida nchini Marekani alipokuwa anapatiwa matibabu.

Manji aliyezaliwa Oktoba 14, 1975 nchini Tanzania, pia aliwahi kuwa Diwani wa Kata ya Mbagala Kuu jijini Dar es Salaam kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Mfanyabiashara huyo atakumbukwa zaidi na wanachama na mashabiki wa timu ya Yanga SC kwani aliirudisha kwenye hadhi yake, baada ya kukumbwa na migogoro mingi.

Aliingia Yanga mwaka 2006 kama mdhamini kupitia kampuni yake moja ya bahati nasibu, baadaye akawa mfadhili Mkuu wa klabu hiyo kabla ya kuwa Mwenyekiti.

Katika kipindi chake cha kuwa mfadhili na Mwenyekiti wa Yanga, Manji atakumbukwa kwa kuirejeshea Yanga hadhi na heshima.

Alipoingia aliikuta Yanga imedhoofu kiuchumi na haiwezi kushindana na mahasimu wao, Simba SC katika kuwania wachezaji bora ambao ndiyo mtaji wa kushinda mataji.

Moja ya wachezaji ambao waliwasajili Yanga kwa kishindo kutoka kwa mahasimu wao wa jadi Simba, ni Emmanuel Okwi, Kelvin Yondani, Juma Kaseja na ikawapora mchezaji Mbuyu Twite ambaye alikuwa ameshatangazwa na Wekundu wa Msimbazi kutokea, APR ya Rwanda, lakini akaibukia Jangwani.

Baada ya mafanikio makubwa, alijiondoa rasmi Yanga mwaka 2017, na kusababisha klabu hiyo kuyumba kiuchumi, na katika kusaka fedha ilianza kuanzisha harambee iliyopachikwa jina la 'bakuli' hadi pale Kampuni ya GSM ilipoingia. Nipashe

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages