NEWS

Monday 1 July 2024

Wafanyabiashara Soko Kuu Musoma waanza mgomo wakiwatuhumu machinga



Moja ya malango ya Soko Kuu la Musoma likiwa limefungwa leo kutokana na mgomo wa wafanyabiashara wa soko hilo wanaoshinikiza machinga wanaolizunguka waondolewe. (Picha na Mwananchi)
------------------------------------------------

Na Mwandishi wa
Mara Online News
--------------------------

Siku chache baada ya wafanyabiashara wa Soko Kuu la Kariakoo jijini Dar es Salaam kusitisha mgomo wa kufungua maduka wakipinga ‘utitiri’ wa kodi, wenzao wa Soko Kuu la Musoma mkoani Mara wamegoma kufungua malango wakishinikiza wafanyabiashara ndogo ndogo (machinga) ‘wanaokinga’ wateja wao waondolewe.

Wafanyabiashara hao wameshuhudiwa wakigoma kuingia sokoni kuanzia asubuhi leo Julai 1, 2024 wakiitaka serikali kuwaondoa machinga wanaendesha shughuli zao nje kuzunguka soko hilo.

Malalamiko yao yamejikita kwenye hoja kwamba baadhi ya machinga wanaendesha biashara zao hadi kwenye malango ya soko hilo na kuuza bidhaa zao kwa wateja ambao wangeweza kuingia sokoni.

Wamesema hali hiyo imesababisha bidhaa zao kwenye maduka na vibanda ndani ya soko hilo kudoda kwa kukosa wateja - wanaoishia kuchangia machinga wanaolizunguka kwa nje.

Kwa upande wao, machinga wanajitetea kuwa wamechagua kuendesha biashara zao nje ya soko hilo kwani ndipo penye watu wengi, na sio kuzuia wateja wanaokwenda kufanya manunuzi ndani ya soko.

Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Dkt Halfan Haule alipoulizwa na waandishi wa habari ameahidi kwenda kuzungumza na wafanyabiashara hao kwa hatua za ufumbuzi.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages