NEWS

Wednesday 22 April 2020

Kituo cha watoto Busega chasaidiwa kukabili corona


KITUO cha kulea watoto cha Bikra Maria kilichopo Lamadi wilayani Busega, Simiyu chenye watoto wenye umri wa kuanzia miezi miwili hadi miaka 18, kimepokea msaada wa vifaa vya kujikinga na maambukizi ya virusi vya corona (COVID-19) na vyakula kutoka JBS Fuel Co. Ltd.

Msaada huo uliokabidhiwa leo Aprili 22, 2020 unahusisha vitakasa mikono, sabuni za maji, ndoo kwa ajili ya kunawia mikono, mahindi na sukari, vyote vyenye thamani ya Sh milioni mbili.

Awali, akikabidhi msaada huo, Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Lucy Sabu, amesema ameguswa kutoa vifaa na vyakula hivyo kuwasaidia watoto hao kipindi hiki cha tahadhari dhidi ya COVID-19.

“Kwa dhati ya moyo wangu nimeamua kuungana na serikali kuhakikisha hakuna maambukizi zaidi ya ugonjwa wa corona, lakini pia mahindi na sukari vitasaidia kwa chakula,” amesema Sabu.

Mkurugenzi huyo amewataka wadau wengine wakiwemo watu binafsi kujitokeza kwa wingi kusaidia makundi yenye mahitaji maalumu katika jamii wakiwemo watoto.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Busega, Tano Mwera, amemshukuru mkurugenzi huyo na kuwaomba wadau wengine kuunga mkono jitihada za serikali katika kudhibiti janga hilo la kimataifa.

Naye Mratibu wa magonjwa yanayosababishwa na virusi vya Corona na Ukimwi Mkoa wa Simiyu, Dkt Khamis Kulemba, ameutaka uongozi wa kituo hicho kuongeza maeneo ya kunawia mikono na kuwasisitiza watoto kunawa mara kwa mara.


Mkuu wa Wilaya ya Busega, Tano Mwera(kushoto) akipokea msaada wa vifaa vya kujikinga na Corona na chakula kwa ajili ya watoto wa kituo cha Bikra Maria kilichopo Lamadi kutoka kwa Mkurugenzi wa kampuni ya JBS C.Ltd Lucy Sabu( kulia)


Mkurugenzi wa kituo hicho, Sista Helena Ntabulwa, amesema kinalea watoto 71 kutoka maeneo mbalimbali nchini wakiwemo waliofiwa wazazi, waliotelekezwa na wenye ulemavu wa ngozi.

Sista Ntabulwa ameipongeza serikali mkoani Simiyu chini ya Mkuu wa Mkoa, Anthony Mtaka, akisema imekuwa bega kwa bega na kituo hicho kwa kusaidiana na wadau mbalimbali wenye mapenzi mema na watoto.

Katika hatua nyingine, mjumbe wa bodi ya kituo hicho, Belensi China, amesema kinakabiliwa na changamoto ya fedha za kugharimia matibabu ya watoto, mishahara ya wafanyakazi na chakula, hivyo kuomba wadau kuendelea kuwasaidia.

(Habari na Anita Balingilaki, Busega)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages