NEWS

Thursday 18 June 2020

Magonjwa yaliyosahaulika kutokomezwa Itilima


WAKAZI 283,972 wa wilaya ya Itilima mkoani Simiyu, wanatarajiwa kunufaika na mradi wa kutokomeza magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele, unaotekekezwa wilayani humo kwa gharama ya shilingi bilioni 1.9.

Hayo yamesemwa Juni 17, 2020 na mtaalamu wa afya na lishe  wa World Vision Tanzania, Dkt Irene Mbugua, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Gilbert Kamanga, wakati wa utambulisho na uzinduzi wa mradi huo wa miaka mitatu (March 2020 hadi Desemba 2022).
Mwenye T-shirt ya kijivu ni mtaalamu wa maji na usafi wa mazingira kutoka makao makuu ya World Vision Tanzania, Rose Riwa, akiwasilisha mada wakati wa utambulisho na uzinduzi wa mradi huo.

 Dkt Mbugua amesema mradi huo unafadhiliwa na Serikali ya Korea Kusini kupitia Shirika la Maendeleo la KOICA na kwamba utatekelezwa kwenye kata zote 22, vijiji 102 na shule za msingi 87 zilizopo wilayani Itilima, walengwa wakiwa ni watoto wenye umri wa kwenda shule, walimu, wahudumu wa afya na wanajamii kwa ujumla.

"Shirika la World Vision kwa kushirikiana na Serikali ya Korea Kusini na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto - kitengo cha kudhibiti magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele (NTDCP), tumeshirikiana ili kudhibiti na ikibidi kutokomeza magonjwa haya, hususan kichocho na minyoo tumbo, lengo kubwa ni kuunga juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano," amesema Dkt Mbugua.
Aliyevaa shati la rangi ya karoti ni Meneja wa World Vision Kanda ya Ziwa, John Massenza, akitoa ufafanuzi kwa washiriki.

Kwa upande wake, mtaalamu wa maji na usafi wa mazingira kutoka makao makuu ya shirika hilo, Rose Riwa, amesema kwa mujibu wa utafiti walioufanya mwaka 2018, mradi huo utapunguza maambukizi mapya na rejea kwa kuongeza umezaji wa dawa za kinga, tiba, kuzuia wadudu waenezao na kuboresha huduma za maji na usafi wa mazingira.

"Matokeo ya utafiti wa awali kuhusu hali ya maji na usafi wa mazingira uliofanywa mwaka 2018 yalionesha kuwa asimilia 51 ya wakazi wa Itilima wanapata maji safi na salama kutoka kwenye vyanzo vya maji 1,031 huku mahitaji yakiwa ni vyanzo 3,672. Asilimia 24 wanatumia vyoo bora na vifaa vya kunawia mikono na asilimia 5.2 hawana vyoo," amesema Riwa.

Naye Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima, Dkt Anold Musiba, amesema maambukizi ya kichocho na minyoo tumbo wilayani humo yapo kwa asilimia 30 na kwamba kumekuwepo na juhudi kubwa za kuhakikisha walengwa wote wanafikiwa.

(Imeandikwa na Anita Balingilaki, Itilima)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages