NEWS

Wednesday 1 November 2023

Watendaji wa mitaa, kata Tarime Mji wapewa maelekezo kudhibiti kipindupindu



Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Tarime, Daniel Komote akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo jana Oktoba 31, 2023. Kushoto ni Katibu Tawala wa Wilaya ya Tarime, Mwl Saul Mwaisenye na kulia ni Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Gimbana Ntavyo.
------------------------------------------

Na Godfrey Marwa, Tarime
Mara Online News
--------------------------
 

BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Tarime mkoani Mara, limewataka watendaji wa mitaa na kata kusimamia usafi wa mazingira ili kudhibiti mlipuko wa kipindupindu. 

“Tunataka mitaa ya mji wetu iwe misafi, Baraza tunatoa maelekezo, watendaji wa mitaa na kata simamieni hilo, ugonjwa wa kipindupindu hauchagui wala haubagui,” Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Daniel Komote alisisitiza katika kikao cha baraza hilo mjini Tarime jana Oktoba 31, 2023. 
Madiwani kikaoni
Naye Mkuu wa Kitengo cha Udhibiti Taka na Usafi wa Mazingira Halmashauri ya Mji wa Tarime, Erasto Mbunga alitoa wito kwa wakazi wa mji huo kwa ujumla kuzingatia kanuni za usafi wa mazingira, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wanajenga vyoo bora. 

“Kama kitengo tumejipanga, tunaendelea na kampeni ya usafi wa mazingira, tunapita kaya kwa kaya kuhakikisha maeneo tunayoishi yanakuwa safi, wanaokiuka maelekezo ya ujenzi wa vyoo bora tunawakamata na kuwapiga faini. Tutakuwa wakali kuhakikisha sheria ndogo ndogo za mazingira zinafuatwa,” Mbunga aliiambia Mara Online News ofisini kwake baada ya kikao hicho. 

Kikao hicho cha Baraza la Madiwani pia kilihudhuriwa na Katibu Tawala wa Wilaya ya Tarime, Mwl Saul Mwaisenye, wakuu wa taasisi na idara mbalimbali za Serikali na viongozi wa chama tawala - CCM. 

#Tunakuhabarisha Ukweli kwa Weledi

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages