NEWS

Friday 29 May 2020

Wanafunzi kidato cha sita walivyojipanga kufanya mtihani


WANAFUNZI wa kidato cha sita waliokuwa likizo mkoani Simiyu, wamepokea kwa furaha tamko la serikali la kufungua shule kuanzia Juni 1, 2020, huku wakisema wamejipanga vizuri kuelekea mtihani wa taifa wa kidato hicho.

Wakizungumza na Mara Online News kwa nyakati tofauti mjini Bariadi, Simiyu Mei 27, 2020, wamesema wameweza kutumia likizo ya dharura iliyoitishwa na serikali kupisha mapambano dhidi ya virusi vya corona, kujiandaa kwa ajili ya mitihani ya mwisho.
 
Thomas Mwambilija
"Ilikuwa nimalize mtihani wangu wa NECTA Mei 22, mwaka huu maana nachukua PCB, lakini virusi vya corona vikaniharibia," amesema Thomas Mwambilija, mwanafunzi wa kidato cha sita katika Shule ya Sekondari ya Wavulana Ihungo iliyopo mkoani Kagera.

Mwambilija ameongeza "Nilikuwa nimejiandaa vya kutosha, corona ilivyoingia ikaharibu kila kitu, lakini naishukuru serikali kwani likizo ya dharura imenisaidia kujiandaa vya kutosha, nimejisomea na nipo tayari kwa mtihani."

Hilda Revocatus, mwanafunzi wa kidato cha sita katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Chief Ihunyo iliyopo mkoani Mara, amesema janga la corona lilitaka kuua ndoto zake, lakini amefurahi shule kufunguliwa na kwamba amejipanga vyema kumalizia vipindi vya masomo vilivyobaki.
 
Hilda Revocatus
Wanafunzi hao pia wameishukuru serikali kipitia Wizara ya Elimu kwa kuunda mpango maalumu uliowawezesha kusoma kwa njia ya mtandao wakiwa likizo nyumbani, ambao umewasaidia kufanya marudio ya masomo yote.

Katika hatua nyingine, wanafunzi hao wamempongeza Rais Dkt John Magufuli kwa hotuba zake mbalimbali ambazo zimesaidia wananchi kupunguza hofu ya corona nchini.

(Imeandikwa na Anita Balingilaki, Bariadi)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages