NEWS

Wednesday 10 June 2020

Takukuru yabaini ufisadi wa mabilioni Nyamongo


Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Mara imebaini ufisadi wa Zaidi Ya shilingi Bilioni 3  katika malipo ya fidia kwa wananchi wa kijiji cha Matongo kilichopo Nyamongo wilayani Tarime, yaliyofanywa na Mgodi wa Dhahabu wa North Mara.
Mkuu wa Mkoa wa Mara Adam Malima(kulia) akitoa maagizo mbalimbali kuhusu ufisadi ambao umefanywa Nyamongo
Taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Mara, Alex Kuhanda kwa waandishi wa habari mjini Tarime leo Juni 10, 2020, imesema Sh 2,127,236,784 ni malipo hewa ya fidia ya nyumba za wananchi hao na Sh 1,143,796,786.28 ni malipo hewa ya posho ya usumbufu wa kuhama kutoka kwenye nyumba hizo.

Kuhanda amesema uchunguzi wa ofisi yake umebaini kwamba malipo stahiki ya fidia kwa wananchi hao ni Sh 226,858,656.52 na siyo Sh 3,482,988,360 zilizolipwa kama fidia ya nyumba hewa 72 za wananchi hao.

Mkuu wa TAKUKURU Mara Alex Kuhanda akieleza udanganyifu katika zoezi la malipo ya fidia
“Uchunguzi wetu bado unaendelea ili kuwabaini hasa wote waliohusika katika mchezo huu mchafu na kiasi zaidi cha fedha kilichohusishwa kama malipo hewa,” amesema mkuu huyo wa Takukuru Mkoa wa Mara.

RPC William Mkonda(kushoto) na RPC Daniel Shilla (kulia) wakiteta baada ya kupokea maagizo ya RC Malima
Kwa upande wake, Mkuu wa MKoa wa Mara, Adam Malima, amewaagiza Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Tarime Rora, William Mkonda na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Daniel Shilla, kuwatia nguvuni wote waliohusika katika ufisadi huo wakiwemo watumishi wa Serikali na viongozi wa vijiji na vitongoji.

“Tuna watendaji wa Serikali, wote wakamatwe na wafunguliwe mashitaka kwa kujaribu kuibia Serikali. Viongozi wa vijiji, viongozi wa vitongoji wote waliohusika wakamatwe,” ameagiza Malima katika kikao hicho.

Alisema uchunguzi zaidi juu ya ufisadi unaohusisha Sh zaidi ya bilioni tano unaendelea na ikibainika hata wafanyakazi wa mgodi wa North Mara unaoendeshwa na kampuni ya Barrick wamehusika watatiwa mbaroni.

“Pia kwenye tasisi za kifedha [benki] uchunguzi ukibaini wamehusika tunawachukua,” ameongeza Malima.

Hata hivyo, mkuu huyo wa mkoa amesema baadhi  ya watuhumiwa wa ufisadi huo wameanza kujisalimisha, huku akiwataka wananchi wote wenye uhakika kuwa maombi ya fidia zao ni halali kuendelea kuchukua noti zao.

(Habari, picha na Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages