NEWS

Saturday 1 August 2020

Samia azitaka benki ziongeze mikopo kwa wakulima



MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu Hassan, amezitaka taasisi za kifedha nchini kuongeza mikopo kwa wakulima kuwawezesha kuongeza uzalishaji, hivyo kukuza pato lao na taifa kwa jumla.

Samia ametoa rai hiyo jana wakati wa uzinduzi wa Maonesho ya 28 Nanenane yanayofanyika kitaifa katika viwanja vya Nyakabindi wilayani Bariadi, Simiyu na kuongeza kuwa katika kipindi kilichopita utoaji wa mikopo kwa sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi ulikuwa asilimia tisa.

Aidha, Makamu huyo wa Rais amewataka watafiti wa mbegu bora kuweka wazi tafiti hizo kwa maafisa ugani kwa ajili ya kuzifikisha kwa wakulima ili kuchochea uzalishaji wa mazao.
Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan (katikati) akisikiliza maelezo kutoka kwa mtaalamu katika mojawapo ya mabanda ya Maonesho ya Nanenane kwenye viwanja vya Nyakabidi

Akizindua jengo la Wizara ya Kilimo katika viwanja hivyo vya maonesho, lililogharimu shilingi milioni 400, Samia amewataka wasimamizi husika kuhakikisha kuwa linatumika katika kuelimisha walengwa.

Awali, akimkaribisha Makamu wa Rais, Waziri wa Kilimo, Japheth Hasunga, amesema wizara hiyo imejipanga kuimarisha upatikanaji wa malighafi kwenye viwanda vya ndani, pembejeo za kilimo, viuadudu na mbolea kwa bei nafuu.

Waziri Hasunga amesema jengo hilo litatumika mwaka mzima kuhamasisha shughuli za kilimo, mifugo na uvuvi, huku akiwasisitiza wananchi kujitokeza kupata elimu itakayowasaidia kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.

“Jengo hili na majengo mengine ya kilimo yatatumika pia kuelimisha wananchi juu ya elimu ya lishe kwa lengo la kukabiliana na udumavu wa akili kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano. Jumla ya watoto milioni tatu wana udumavu wa akili… mikoa inayoongoza kwa uzalishaji wa chakula ndio yenye idadi kubwa ya watoto wenye tatizo hilo,” amesema.
Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan (katikati) akiendelea kutembelea mabanda ya bidhaa katika Maonesho ya Nanenane kwenye viwanja vya Nyakabindi

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka, ameziomba wizara za Kilimo, Mifugo na Uvuvi kuangalia uwezekano wa kuanzisha kituo maalumu kitakachowezesha wananchi kujifunza teknolojia mbalimbali za kilimo, ufugaji na uvuvi.

Maonesho ya Nanenane yanafanyika kitaifa mkoani Simiyu kwa miaka mitatu mfululizo ambapo kaulimbiu ya mwaka huu inasema “Kwa Maendeleo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Chagua Viongozi Bora 2020”.

(Imeandikwa na Anita Balingilaki, Bariadi)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages