NEWS

Saturday 19 September 2020

Waziri Mkuu awataka wakurugenzi kuongeza ubuni miradi ya maendeleo

 

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akihutubia mkutano wa hadhara wa kampeni za ubunge Itilima mkoani Simiyu, jana.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu (CC) na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa, amewataka wakurugenzi watendaji wa halmashauri nchini kuendelea kuwa wabunifu wa miradi ya kimaendeleo kwenye halmashauri zao ili kuongeza mapato ya ndani.

Mbali na hilo amewaomba wananchi ambao ni wanachama wa CCM na wa vyama vingine na wasio na vyama kuwachagua wagombea wa CCM wa nafasi za urais, ubunge na udiwani ili waende kutekeleza miradi mbalimbali ya kimaendeleo.

Umati wa wananchi ukimsikiliza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa (hayupo pichani) katika mkutano wa uzinduzi wa kampeni za ubunge jimbo la Itilima, jana.

 

Majaliwa ameyabainisha hayo jana wakati wa uzinduzi wa kampeni za ubunge jimbo la Itilima, Njalu Silanga (CCM), ulifanyika kwenye viwanja vya Lagangabilili - itilima mkoani simiyu.

"Itilima ya sasa inapendeza sana ndani ya kipindi cha miaka mitano makao makuu yanapendeza, yana majengo ya kisasa yenye miundombinu ya kisasa, wananchi tuchagueni tuendelee kuwaletea maendeleo na tuna mkakati wa kujenga maghala ya chakula kwenye maeneo yote yanayozalisha chakula kwa wingi," amesema Waziri Mkuu, Majaliwa.

Aidha, amewataka wananchi kuitunza amani ya nchi hasa tunapoelekea kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 28, mwaka huu huku akiwaomba kutumia haki yao ya kikatiba ya kuwachagua viongozi watakaoleta maendeleo.

Kwa upande wake, mgombea ubunge jimbo la Itilima, Silanga, amemhakikishia Waziri Mkuu ushindi wa kishindo kwa wagombea wote wa chama hicho kuanzia nafasi ya urais, ubunge na udiwani kutokana na utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020 kwa vitendo na kwa wakati.

"CCM tunaendesha kazi zetu kwa kufuata ilani inasemaje, nami nafuata ilani inavyosema na hii haina ubishi wana-Itilima ahadi za awamu ya tano zimetekelezwa kuanzia kwenye sekta ya afya na elimu, wana-Itilima tumetendewa haki, nipeni miaka mitano tena tuendelee kusogeza maendeleo, ndani ya kipindi changu huwezi kulinganisha na kipindi kile jimbo lilipokuwa upinzani, siku ya kupiga kura naombeni mnichaguea mimi niwatumikie,"  amesema Silanga.

Sehemu nyingine ya wananchi waliojitokeza kwenye mkutano wa uzinduzi wa kampeni za ubunge jimbo la Itilima mkoani Simiyu juzi, uliohutubiwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa (hayupo pichani).

 

(Habari na picha zote na Anita Balingilaki, Itilima)

 

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages