NEWS

Saturday, 23 May 2026

Grumeti Fund washiriki uzinduzi Mfuko wa Waandishi wa Habari Mara



Mgeni rasmi, Dkt. Khalfan Haule (kushoto), akimkabidhi cheti cha shukrani kwa Afisa Mahusiano wa Grumeti Fund, Domina Mlegwa, katika hafla ya uzinduzi wa Mfuko wa Waandishi wa Habari Mkoa wa Mara jana. Kulia ni Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa, Jacob Mugini.

Na Mwandishi Wetu
Tarime
------------

Grumeti Fund ni miongoni mwa wadau walioshiriki katika uzinduzi wa Mfuko wa Waandishi wa Habari Mkoa wa Mara, uliofanyika sambamba na maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari mkoani humo.

Hafla ya uzinduzi na maadhimisho hayo ilifanyika jana Mei 22, 2026 katika Hotel ya CMG mjini Tarime, ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Mara, Kanali Evans Mtambi, ambaye aliwakilishwa na Mkuu wa Wilaya ya Rorya, Dkt. Khalfan Haule.
Mgeni rasmi akizindua Mfuko wa Waandishi wa Habari Mkoa wa Mara.

Grumeti Fund iliwakilishwa na Afisa Mahusiano wake, Domina Mlegwa, ambaye alitumia fursa hiyo kueleza inavyoshiriki katika shughuli za uhifadhi wa wanyamapori na kuchangia maendeleo ya jamii zinazozunguka maeneo ya shughuli zake katika wilaya za Serengeti na Bunda .

Domina alisema shirika hilo linatambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari katika kuhamasisha uhifadhi wa wanyamapori, kukuza utalii na kuhamasisha maendeleo ya jamii.

Alisema Grumeti Fund itaendelea kushirikiana na waandishi wa habari katika shughuli zake, zikiwemo za kuhamasisha ulinzi na uhifadhi wa wanyamapori, maendeleo ya jamii zinazoizunguka katika wilaya za Serengeti na Bunda mkoani Mara na taifa kwa ujumla.

Grumeti Fund ni Shirika lisilo la Kiserikali linalosaidia uhifadhi wa wanyamapori na maendeleo ya jamii katika vijiji vilivyo jirani na Mapori ya Akiba ya Ikorongo-Grumeti ambayo ni sehemu ya ikolojia ya Serengeti.

Domina akizungumza katika hafla hiyo.

Wadau wengine walioshiriki uzinduzi na maadhimisho hayo ni kutoka Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara, Kemanyanki Group,  WAMACU Ltd, Hope of Girls and Women in Tanzania, Soya One Limited na TANAPA,  na Jeshi la Polisi, miongoni mwa wengine, ambapo wote walilitunukiwa vyeti vya shukrani.

Wadau hao walipewa nafasi ya kuzungumza mmoja baada ya mwingine, ambapo pamoja na mambo mengine, waliahidi kuendelea kushirikiana na waandishi wa habari katika kuchochea maendeleo ya jamii na taifa.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, Dkt. Haule alisema serikali inatambua na kuthamini umuhimu wa waandishi wa habari na mchango wao katika kuandika habari zinazohamasisha maendeleo na kutangaza fursa za uwekezaji zilizopo mkoani Mara.

Aidha, Dkt. Haule alitumia fursa hiyo pia kuwasisitiza waandishi wa habari kuendelea kuandika habari zinazohamasisha amani, umoja na upendo kwa maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla.
Viongozi na wadau katika picha ya pamoja.

Katika kuunga mkono Mfuko wa Waandishi wa Habari Mkoa wa Mara, Mkuu wa Mkoa, Kanali Mtambi, aliahidi kuchangia shilingi milioni mbili ili kuutunisha.

Awali, Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Mara, Jacob Mugini, aliwashukuru wadau wote walioitikia mwito wa kuunga mkono juhudi hizo za waandishi wa habari, huku akiwaahidi ushirikiano kwa maslahi mapana ya jamii na taifa.
Viongozi\, wadau na baadhi ya waandishi wa habari katika picha ya pamoja. (Picha zote na Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages