NEWS

Friday, 26 June 2026

Utajiri wa wanyamapori Tanzania waivutia Afrika, dunia



Simba wakifurahia mazingira hai katika Hifadhi ya Taifa Serengeti

Na Mwandishi Wetu
Arusha
--------------

Kwa kipindi cha miaka 10 iliyopita, sekta ya wanyamapori nchini imegeuka kuwa kivutio kikubwa cha utalii barani Afrika na duniani kote kutokana na ongezeko la idadi ya wanyama hao mwaka hadi mwaka.

Ongezeko hilo ni kwa mujibu wa sensa ya kitaifa iliyofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) mwaka 2024/2025.

Ripoti ya matokeo ya sensa hiyo ilitolewa hadharani hivi karibuni jijini Arusha na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji.

Waziri Kijaji alisema mbele ya viongozi mbalimbali wa taasisi zinazoshughulika na sekta ya uhifadhi kwamba ongezeko la wanyamapori linatokana na usimamizi na ulinzi madhubuti wa Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kwa kushirikiana na taasisi nyingine za kitaifa.

Alisema Tanzania sasa inashika nafasi ya kwanza barani Afrika kwa kuwa na nyati (mbogo) 324,437 na simba wapatao 17,200.

Aliongeza kuwa taifa hili kubwa la Afrika Mashariki linashika nafasi ya tatu na ya nne barani Afrika kwa kuwa na tembo 66,700 na faru weusi na weupe 302.

Dkt. Kijaji aliitumia nafasi hiyo pia kusifu jitihada kubwa za uhifadhi na ulinzi wa wanyamapori zilizofanywa na Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCAA), Mamlaka ya Wanyamapori na Huduma ya Misitu, pamoja na taasisi nyingine za kitaifa zinazohusika na ujenzi wa sekta imara ya utalii.

Uhifadhi na ulinzi bora wa wanyamapori, Waziri Kijaji alisema umechangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa sekta ya utalii duniani na kuwepo kwa mwelekeo chanya wa mfumo wa ikolojia nchini Tanzania.

Naye Mkurugenzi wa TAWIRI, Dkt. Eblate Mjingo, alisema sensa ya 2024/2025 imeonesha kuwepo kwa aina 28 za wanyamapori wa kati na wakubwa katika mifumo yote ya ikolojia ikilinganishwa na miaka 10 iliyopita.

Dkt. Mjingo alieleza kuwa wanyamapori walioongezeka kwa wingi ni pamoja na tembo, nyati, faru, simba, twiga, nyumbu na tandala.

Takwimu za sensa hiyo zinaonesha kuwa hifadhi sita zenye idadi kubwa ya wanyamapori ni Serengeti, Ruaha, Nyerere, Mikumi, Tarangire na Katavi.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages