NEWS

Thursday, 20 August 2026

Tarime: Huduma ya maji safi yarejea Bomani baada ya MUWASA kuzibua bomba lililokuwa limeziba



Mkazi wa mtaa wa Bomani, wilaya ya Tarime mkoani Mara, akifurahia huduma ya maji safi ya bomba nyumbani kwake kama alivyokutwa na camera ya Mara Online News, jana Jumatano.

Na Mwandishi Wetu
Tarime
------------

Wakazi wa mtaa wa Bomani, wilaya ya Tarime mkoani Mara, wamethibitisha kuendelea kupata maji safi ya bomba bila, baada ya Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Musoma (MUWASA) kuzibua bomba lililokuwa limeziba na kusababisha baadhi ya wateja kukosa huduma hiyo kwa siku kadhaa.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na MUWASA, matengenezo hayo ambayo yalifanyika Agosti 18, 2026 pia yalisababisha maji kuchanganyikana na tope ambalo lilibadilisha uhalisia wa rangi ya maji katika eneo hilo,

Hata hivyo, kumekuwa na picha mjongeo iliyosambazwa kwenye mitandao ya kijamii ikionesha kuwa maji yakitoka kwenye bomba yakiwa na rangi isiyokuwa ya kawaida hata baada ya huduma ya maji safi kurejea.

Habari njema ni kwamba wakazi wa mtaa wa Bomani walizungumza na Mara Online News kwa nyakati tofauti jana Jumatano na kuthibitisha kuwa kwa sasa mabomba yanatoa maji safi na wanaendelea kupata huduma hiyo kama kawaida.

Aidha, uongozi wa MUWASA) ulifika katika mtaa wa Bomani jana Jumatano na kufanya ufuatiliaji wa hali halisi ya huduma ya maji ya bomba.
Katika ziara hiyo, uongozi wa MUWASA ulishuhudia na kujiridhisha kuwa wakazi wa mtaa huo wanaendelea kupata huduma ya maji safi na salama ya bomba kama kawaida.

"Mimi kwangu ninapata maji masafi, machafru sijayaona. Kama kuna mtu kwake maji yanatoka machafu, afuatilie vizuri, labda laini yake imetoboka,” alisema mkazi wa mtaa wa Bomani aliyejitambulisha kwa jina la Mama Monica.
Mama Monica

Mkazi mwingine wa mtaa huo, Ester Athanas Pascal, naye alithibitisha upatikanai wa huduma ya maji safi ya bomba nyumbani kwake. "Sioni changamoto yoyote hapa kwangu, ukifungulia bomba maji yapo, sioni shida,” alisema.

Mwingine aliyejitambulisha kwa jina la Andieli, alisema: "Kwangu sioni tatizo kwenye maji, yanapatikana na ni masafi.”

Naye Kambarage Mantago, alisema: "Hapa Bomani mimi naona maji yako sawa, kwangu ninapata maji saa zote mpaka chooni, na ninalipa bili yangu kwa wakati.”
Kambarage Mantago

Ushuhuda huo wa wakazi wa mtaa wa Bomani umeonesha picha tofauti na taswira iliyojengwa na taarifa iliyosambazwa mitandaoni.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages