NEWS

Sunday 24 May 2020

SIMIYU: TUMEJIPANGA KUPOKEA KIDATO CHA SITA

Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Jumanne Sagini
MKOA wa Simiyu umejipanga kuwapokea wanafunzi wa kidato cha sita kuanzia June mosi, 2020 kama ilivyoelekezwa na Rais Dkt John Magufuli.

Akizungumza na waandishi wa habari Mei 23, 2020, Katibu Tawala wa mkoa huo, Jumanne Sagini amesema serikali mkoani humo imejipanga pia kutumia vizuri siku 28 zilizotolewa na wizara yenye dhamana ya elimu kufanya maandalizi ya mtihani wa taifa wa kidato hicho utakaoanza Juni 29, 2020.

“Elimu ni kipaumbele cha kwanza mkoani kwetu, tumejipanga kikamilifu kuwapokea vijana wetu wa kidato cha sita, tuliandaa mkakati wa kuwasaidia kujisomea wakati wa likizo ya tahadhari ya corona,” amesema Sagini na kuongeza:

“Viongozi katika maeneo yote watahakikisha tahadhari zote zinazotolewa na wizara yenye dhamana na afya katika kujikinga na maambukizi ya virusi vya corona yanazingatiwa.”

Ametoa wito kwa wazazi na walezi mkoani humo kuendelea kusimamia na kuhimiza watoto ambao bado wako likizo ya dharura kujisomea mpaka shule zitakapofunguliwa.

Afisa Elimu Mkoa wa Simiyu, Mwalimu Ernest Hinju, amesema kipindi hiki cha likizo ya dharura wanafunzi wamekuwa wakijisomea, kufanya majaribio na kurudia mada ambazo hazikueleweka vizuri.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Fabian Manoza, amesema wamejipanga kuhakikisha wanakamilisha kwa wakati mahitaji yote ya kimasomo kwa wanafunzi wa kidato cha sita kuwawezesha kujiandaa kwa ajili ya mtihani wa taifa.

Mkoa wa Simiyu una wanafunzi 953 wanaotarajiwa kufanya mtiani wa kuhitimu kidato sita kuanzia June 29, 2020.

                                  (Imeandikwa na Anita Balingilaki, Simiyu)



No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages