NEWS

Monday 25 May 2020

CCM yaifuta Chadema Tarime


CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) sasa kimebaki historia wilaya ya Tarime baada ya Katibu wake, Samwel Mgaya kufuata nyayo za Mwenyekiti wake, Mwita Joseph kukihama na kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Kwa hatua hiyo, ni wazi kwamba Chadema sasa kimebaki bila mwenyekiti na katibu wa wilaya ya Tarime mkoani Mara.

Mgaya ametangaza kuhamia CCM leo Mei 25, 2020 ikiwa ni takriban mwezi umepita tangu Joseph atimkie kwenye chama hicho tawala kwa maelezo ya kutoridhishwa na mwenendo wa uongozi wa juu wa Chadema.

Akizungumza mbele ya Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Tarime, Daudi Ngicho na Naibu Waziri mwenye dhamana ya Tamisemi, Mwita Waitara, Mgaya amesema ameamua kuhamia chama hicho tawala kwa hiari yake.

“Nimetafakari… nimekuja kuungana nanyi [CCM] kumuunga mkono Rais John Magufuli, mambo [akimaanisha maendeleo] anayofanya sasa hivi hata kama ni mtoto mdogo anayaelewa,” amesema Mgaya.
Samweli Mgaya (katikati) akiwa amevalia sare za CCM mara baada ya kujiunga na chama hicho. Kulia ni Mwenyekiti wa CCM Wilaya, Daudi Ngicho na kushoto ni Katibu wa chama hicho wilayani, Hamis Mkaruka.
Akizungumza wakati wa mapokezi hayo ofisini kwake mjini Tarime, Mwenyekiti wa CCM Wilaya, Ngicho, amesema Mgaya na Joseph ni wapiganaji wazuri na amewakaribisha kuungana na wanachama wa chama hicho katika kusukuma gurudumu la maendeleo ya Watanzania.

Naye Naibu Waziri Waitara ambaye pia ni Mbunge wa Ukonga mkoani Dar es Salaam, amesema CCM kimepata watu muhimu [Joseph na Mgaya] na kutuma salamu kwa Chadema kwamba kitarajie kuporomoka zaidi.

“Watu wametambua kazi nzuri inayofanywa na Rais Dkt John Magufuli, malalamiko mengi ya wananchi yameshughulikiwa, hii ni serikali sikivu,” amesema Waitara.
Naibu Waziri wa TAMISEMI na kada wa CCM, Mwita Waitara akisisitiza jambo wakati wa mapokezi ya Katibu wa Chadema Wilaya ya Tarime, Samwel Mgaya (hayupo pichani)


Wengine walioungana na Mgaya kuhamia CCM leo, vyama na kata wanakotoka wilayani Tarime vikiwa kwenye mabano ni Nashon Mchuma (Chadema, Gwitiryo), Boniphace Mataro (Chadema, Matongo), Emmanuel Marwa (Chadema, Nyamwaga) na George Nyanchama (ACT – Wazalendo, Nyandoto).

Hata hivyo, Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Mara, Lucas Ngoto amesema chama hicho kiko imara kwani wanaohama ni viongozi lakini wanachama wapo wengi wanaoweza kuziba nafasi za uenyekiti na ukatibu zilizoachwa wazi wilayani Tarime.

(Imeandikwa na Waitara Meng’anyi, Tarime)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages