NEWS

Monday 5 October 2020

Simiyu watenga mamilioni kuzawadia watakaong’ara mtihani darasa la saba

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka akizungumza na baadhi ya wanafunzi watakaofanya mtihani wa taifa wa kuhitimu darasa la saba mkoani humo.

 

MKUU wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka ametangaza zawadi kwa wanafunzi watakaofanya vizuri kwenye mtihani mtihani wa taifa wa kuhitimu darasa la saba utakaoanza nchini kote kesho Jumatano.

Mbali na wanafunzi pia Mtaka ametangaza zawadi kwa walimu, shule na wilaya ambazo zitaingia kumi bora kitaifa katika mtihani huo ambao unatarajiwa kufanyika Oktoba 7 na 8, 2020.

"Mkoa umeandaa shilingi milioni tano zawadi kwa wanafunzi watakaofanya vizuri kwenye mtihani huo na kuingia 10 bora kitaifa ambapo kila mwanafunzi atapatiwa Sh. 500,000 na mbali na hilo kwa walimu mkoa umeandaa zawadi pia, mwalimu ambaye somo lake litapata alama A nyingi atajipatia shilingi 500,000,” alisema Mtaka.

Mtaka ameyasema hayo jana Jumatatu mbele ya wanafunzi wa darasa la saba na walimu wa shule za msingi Sima na Somanda zilizopo Halmashauri ya Mji wa Bariadi mkoani Simiyu wakati wa ziara yake kuangalia maandalizi kabla ya kufanyika kwa mtihani huo.

Kuhusu shule itakayoingia kumi bora kitaifa, mkuu huyo wa mkoa amesema itapatiwa shilingi milioni tatu, huku wilaya itayoingia 10 bora kitaifa walimu wake watapata fursa ya kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

“Zawadi hizi ni motisha kwa walimu na wanafunzi ambazo mkoa umekuwa ukitoa kila mwaka, katika kuhakikisha unaendelea kufanya vizuri kwenye mitihani yote na tumefanya hivi mwaka huu kwa wanafunzi na walimu wa kidato cha sita baada ya mkoa kushika nafasi ya tatu kitaifa… mkoa umejipanga kuhakikisha unatoa motisha ya kutosha kwa walimu na wanafunzi.

"Niendelee kuwasisitiza viongozi wote wa mkoa kuwaheshimu walimu na kuwatatulia changamoto zao kwa haraka, na walimu toeni taarifa kwangu kama atakuwepo kiongozi yeyote anayewanyanyasa," amesema Mtaka.

Kwa upande wake, Afisa Elimu Mkoa wa Simiyu, Ernest Hinju amesema watahiniwa 30,779 watafanya mtihani huo mkoani humo,  maandalizi yote yamekamilika na kwamba wana uhakika kuwa lengo la mkoa kushika nafasi ya kwanza kitaifa litafikiwa.

Nao baadhi ya wanafunzi wamesema wamejipanga vyema kuhakikisha wanashika nafasi ya kwanza kitaifa, kwani wameandaliwa vyema na walimu wao kupitia kambi za kitaaluma.

(Imeandikwa na Anita Balingilaki, Simiyu)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages