NEWS

Saturday, 21 December 2024

Nyambari, Maswi wabeba harambee ya Kurya Social Group, zaidi ya milioni 20/- zapatikana Namba Tatu akimwakilisha mgeni rasmi



Nyambari Nyangwine na Eliakim Maswi
------------------------------------

Na Mwandishi Wetu/ Mara Online News

Shilingi zaidi ya milioni 20 zimepatikana katika harambee ya kuchangia uanzishaji wa SACCOS ya Kundi la Kijamii lijulikanalo kama Kurya Social Group (KSG), huku wachangiaji wakuu wakiwa Nyambari Nyangwine na Eliakim Maswi.

Harambee hiyo ilifanyika jana Desemba 20, 2024 katika Hoteli ya Goldland mjini Tarime, Mara.
Viongozi na wanachama wa Kurya Social Group katika picha ya pamoja jana.
----------------------------------

Nyangwine ambaye aliwakilishwa na Mwenyekiti Mstaafu wa CCM Mkoa wa Mara, Samwel Kiboye “Namba Tatu” kama mgeni rasmi katika harambee hiyo, alichangia shilingi milioni 6.5 na Maswi (shilingi milioni 6).

Nyangwine na Maswi wote ni makada wa chama tawala - CCM, na wanatajwa kama wadau wakubwa wa muda wote wa maendeleo ya kijamii katika wilaya ya Tarime.

Nyangwine ambaye ni mfanyabiashara, mwandishi na mchapishaji wa vitabu maarufu nchini, aliwahi kuwa Mbunge wa Jimbo la Tarime mwaka 2010 hadi 2015.

Akizungumza katika harambee hiyo, Namba Tatu aliwasilisha salamu za Nyangwine za kuwashukuru wana-KSG kwa kumwalika kuwa mgeni rasmi na kuwatakia mkutano wenye mafanikio na baraka tele.

“Nyambari Nyangwine ameahidi kushirikiana nanyi kwa kila hali kwa manufaa ya jamii. Mungu awabariki,” Namba Tatu aliwambia wana-KSG.

Samwel Kiboye "Namba Tatu” akimwakilisha Nyambari Nyangwine kama mgeni rasmi katika mkutano wa harambee hiyo.
-----------------------------------

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kurya Social Group, Lucas Magoti alimshukuru Nyangwine na wadau wengine kwa michango yao ya dhati katika harambee hiyo.

"Tunawashukuru sana waliochangia hii SACCOS akiwemo Nyambari Nyangwine, Eliakim Maswi, Chonchorio na wengine wote. Tunakaribisha watu wengine waje kujiungana na group hili,” alisema Magoti.

Naye Mwasisi wa KSG, Martin Marwa alisema uanzishaji wa SACCOS utakuwa hatua muhimu ya kundi hilo katika kuelekea kwenye maendeleo.

Katika hatua nyingine, wanachama wa KSG kwa kauli moja waliazimia kuanza kusaidia watoto walio katika mazingira magumu, wakiwemo yatima kupata elimu ili waweze kutimiza ndoto zao.


Kulikuwa na chakula cha kutosha pia.
(Picha zote na Mara Online News)
---------------------------------
Read Also Section Example

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages