NEWS

Friday 1 May 2020

KANISA LATOA MSAADA KWA KAYA 200 KUKABILI CORONA


Jumla ya kaya 200 zilizopo katika kata ya Nyashimo wilayani Busega mkoani Simiyu zimenufaika na msaada wa vifaa kinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya corona.

Vifaa hivyo vyenye thamani ya shilingi milioni 4.5 zikiwemo ndoo za kunawia mikono 200 , barakoa na sabuni chupa 200 vimetolewa na kanisa la Mennonite tawi la Nyashimo,Busega  kwa ushirikiano na shirika la compassion international Tanzania .

Awali akiongea kwa niaba ya wananchi wa kata ya Nyashimo diwani wa kata hiyo Mickness Mahela amesema kuwa msaada huo umekuja wakati muafaka kwani utawasaidia wananchi katika kukabiliana na janga la Corona .
Mchungaji kiongozi wa kanisa la Mennonite Alfravian Mandago (Kushoto) akikabidhi msaada wa ndooo za kunawia kwa  diwani wa kata ya Nyashimo Mickness Mahela. (Kulia) katikati ni mmoja wa wakazi wa Nyashimo

"msaada huu utawasaidia sana wananchi kwani wamepata uhakika wa kunawa maji tiririka kupitia hizi ndoo ambazo zimetolewa .. binafsi niwapongeze sana kanisa na shirika kwa msaada huu"alisema diwani huyo nakuongeza kuwa:

"nipende kuwakaribisha wengine kuendelea kuiunga mkono Serikali yetu ya awamu ya tano katika kukabiliana na janga hili "aliongeza

Akikabidhi vifaa hivyo mchungaji kiongozi wa kanisa la Mennonite kata ya Nyashimo ,Busega Alfravian Jonh Mandago aliwataka wananchi waliopatiwa vifaa hivyo kuvitumia kwa malengo yaliyokusudiwa na sikubadili matumizi.

"vifaa hivi tulivyovitoa leo ningependa vitumike vizuri si kuvibadilishia matumizi tumetoa ndoo za kunawia mikono zitumike kunawia mikono na si vinginevyo na endapo sabuni hizi zitaisha tumieni sabuni zingine kunawia mikono kikubwa hapa fateni maelekezo na taratibu zinazotolewa na serikali yetu" alisema mchungaji Mandago.

Mbali na msaada huu pia kanisa hilo limetoa barakoa na vitakasa mikono kwa watendakazi wa kanisa wanaotoa huduma za kiroho kwenye jamii lengo likiwa kuwakinga wao na jamii wanayoipelekea huduma ya kiroho dhidi ya maambukizi ya corona.


(Habari Na Anita Balingilaki -  Busega)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages