NEWS

Tuesday 16 June 2020

Madaraka Nyerere atangaza kuwania ubunge Butiama


MTOTO wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Madaraka Nyerere, ametangaza kuwania nafasi ya ubunge katika jimbo la Butiama mkoani Mara, kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Madaraka ametangaza nia hiyo leo Jumanne Juni 16, 2020 nyumbani kwake Mwitongo, Butiama saa chache baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt John Magufuli kuvunja Bunge kupisha michakato ya Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.

“Sijatumwa na mtu yeyote kuomba nafasi hii ila nimejipima uzoefu na uwezo wangu na kuamua kuwa ni wakati muafaka sasa wa kutumia uwezo na uzoefu huo kutumikia jamii pana zaidi,” mtoto huyo wa Baba wa Taifa amewaambia waandishi wa habari.

“Ni kwa sababu sijatumwa na mtu ndio maana leo hii mnaniona niko hapa peke yangu kutoa tamko hili, kwa sababu pamoja na kwamba nahitaji uungwaji mkono wa Chama Cha Mapinduzi na wapigakura wa Butiama, hatua ya kwanza ninataka kuifanya mwenyewe kwa kuamini kwamba ninaweza kupokea majukumu nitakayokabidhiwa.”
Madaraka Nyerere akitangaza nia ya kugombea ubunge katika jimbo la Butiama mbele ya waandishi wa habari nyumbani kwao Mwitongo, Butiama leo Juni 16, 2020, saa chache baada ya Rais Dkt John Magufuli kuvunja Bunge jijini Dodoma.

Amesema jambo la kwanza lililomsukuma kuwania nafasi hiyo ni baada ya kuona Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Magufuli amejenga mazingira mazuri yanayomwezesha mwanachama yeyote wa chama hicho kugombea uongozi na kupata haki bila kujali uwezo wake wa kifedha wala ukaribu wake na viongozi wa juu.

“Pili, Mheshimiwa Magufuli ni kiongozi ambaye tumeona ameweka jitihada kubwa sana za kutanguliza maslahi ya Taifa mbele, kwa hiyo katika mazingira kama hayo na mimi nikijipima na imani zangu nafikiri itakuwa ni heshima kubwa sana ya kufanya kazi pamoja na kiongozi kama huyo kwa sababu naamini yale anayoamini yeye… naweza kuwa askari mzuri wa kufanya naye kazi,” ameongeza Madaraka.

Mbunge wa jimbo la Butiama aliyemaliza muda wake ni Nimrodi Mkono (CCM).

(Imeandikwa na Christopher Gamaina, Butiama)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages