
Tundu Lissu na Freeman Mbowe
Kitendawili cha nani ataibuka mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa kitateguliwa kesho Jumanne baada ya miamba wa siasa; Freeman Mbowe na Tundu Lissu kumenyana katika Mkutano Mkuu wa chama hicho kikuu cha upinzani Tanzania.
Mbowe anatarajiwa kutetea kiti hicho dhidi ya Lissu ambaye alikuwa makamu wake, na ushindani mkali kuwahi kutokea ndani ya chama hicho unatabiriwa katika uchaguzi huo.
Uchaguzi huo unatazamiwa kuwa wa mustakabali wa chama hicho cha upinzani, hasa katika muktadha wa siasa za ndani ya nchi.
Lissu ambaye alirejea kutoka uhamishoni nchini Ubelgiji na kutangaza nia ya kugombea nafasi hiyo, anaungwa mkono na baadhi ya vigogo wa CHADEMA, huku Mbowe akionesha kuwa bado ni kiongozi mwenye mvuto mkubwa katika maeneo mengi ya chama hicho.
Mjadala mkubwa unaendelea kuhusiana na mikakati ya wagombea hao, lakini ni dhahiri kuwa kesho kutakuwa na mvutano mkubwa, kwani kura zitapigwa na matokeo yatakayotangazwa yatatoa mwelekeo wa hatua inayofuata kwa chama hicho kikongwe cha upinzani Tanzania.
Watu wengi ndani na nje ya nchi wanasubiri kwa shauku kubwa kuona nani atashinda kiti hicho na kuongoza CHADEMA kuanzia kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani nchini.
UNAWEZA PIA KUSOMA:
>>Maamuzi: Mkutano Mkuu CCM wawateua Samia, Mwinyi kugombea urais 2025
>>Donald Trump kuapishwa rasmi leo kuwa Rais wa Marekani kwa mara nyingine
>>Dodoma: Stephen Wasira achaguliwa kwa kishindo kuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara
>>HABARI PICHA:Nyambari Nyangwine ndani ya Mkutano Mkuu Maalum wa CCM Taifa jijini Dodoma
No comments:
Post a Comment