NEWS

Wednesday 29 April 2020

KUSAYA ATAKA SUMA JKT KUHARAKISHA UJENZI WA JENGO LA WIZARA YA KILIMO


Katibu mkuu wizara ya kilimo  Gerald Kusaya akiwa  watendaji wa serikali mara  baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la wizara ya kilimo linalojengwa katika viwanja vya Nane Nane Nyakabindi wilayani Bariadi mkoani Simiyu.

Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Gerald Musabila Kusaya  amesema hajaridhishwa na kasi ya ujenzi wa jengo la Wizara ya Kilimo linalojengwa viwanja vya nane nane nyakabindi Bariadi, Simiyu.

Aidha Kusaya amemtaka mkandarasi  ambaye ni Suma JKT kuhakikisha ujenzi unakamilika kabla ya Mei 30, 2020.

Ujenzi wa jengo hilo ulianza mwaka jana 2019  na lilitakiwa kukamilika machi 30 na hadi sasa limefikia asilimia 70 ya ujenzi huku changamoto ikitajwa kuwa ni mabadiliko ya mchoro.

Katika hatua nyingine  katibu mkuu huyo amewahakikishia wanunuzi wa pamba, viongozi wa chama na serikali mkoani Simiyu kuwa madeni yote yatalipwa kabla ya msimu mpya haujaanza.

Ameyasema hayo leo kwa nyakati tofauti kwenye  ziara yake ya siku moja mkoani hapo iliyokuwa na lengo la kuangalia maandalizi ya ufunguzi wa maonyesho ya wakulima kitaifa (Nanenane) na alipotembelea kiwanda cha kuchambua pamba cha alliance kilichopo wilayani Bariadi.

Amesema kuwa serikali haitatangaza kuanza kwa msimu mwingine wakati bado kuna wakulima wanadai, nakuongeza kuwa  wanafanya jitihada zote kuhakikisha wakulima wanalipwa ikiwa ni pamoja na ushuru mwingine wote ukiwemo wa halmashauri na Amcos.


" Yapo mazungumzo yanaendelea, niwahakikishie kuwa deni lote litalipwa hatutangia kwenye msimu mpya wakati bado kuna wakulima wanadai pesa zao za msimu uliopita,"alisema Kusaya.

Anthony Mtaka ni mkuu wa mkoa huo amesema jumla ya madeni yote  ni kiasi cha shilingi bilioni 8.9 huku wakulima peke yao wakidai zaidi ya bilioni 3, na  kiasi kingine kilichobaki kikiwa  madeni ya halmashauri na Amcos.


"zaidi ya wakulima 7000 katika Mkoa huo bado wanadai hela ya pamba yao, kilo milioni 2.6 za pamba  zinadaiwa alisema Mtaka na kuongeza kuwa:


"Wizara ya kilimo ni vema  mkafanya utafiti wa kina kwanza kabla ya kutangaza bei elekezi ya pamba, "aliongeza Mtaka

Kwa upande wake mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Simiyu Enock Yakobo ameitaka serikali kutimiza ahadi hiyo huku akiongeza kuwa  kila wakiingia vijiji jambo linalozungumzwa na  wakulima ni madeni ya pamba  na hivyo kuitaka  serikali kulilipa kabla ya kuingia kwenye uchaguzi mkuu.

Awali akisoma taarifa  katibu wanunuzi wa pamba nchini  Boaz Ogolla alisema kuwa kabla ya kuanza msimu wa ununuzi uliopita walikaa vikao mbalimbali na serikali na kuwekeana makubaliano ya jinsi ya kununua pamba.

Ogolla alisema bei ambayo ilitangazwa na serikali haikuendana na bei ya soko la dunia hali ambayo ilikuwa ikiwangiza katika hasara lakini serikali iliwahidi kuwa itafidia hasara ambayo itatokea kutokana na bei katika soko la dunia kushuka huku ikiwasisitiza wanunuzi waendelee kununua kwa bei ambayo ilikuwa imetengazwa.

" Wanunuzi tulitii hilo agizo, na kununua pamba kwa hasara, tukiwa na imani kuwa serikali itatekeleza ahadi yake ya kufidia hasara ambayo tulipata, na kweli wanunuzi waliuza kwa hasara tunaomba serikali itufidie hiyo hasara," alisema Ogolla.

Madeni hayo ni ya msimu uliopita 2018/19 ambayo yanahusisha madeni ya wakulima , ushuru wa halmashauri, mfuko wa kuendeleza zao hilo (CDTF) pamoja na ushuru wa chama vya msingi vya ushirika vya msingi( Amcos )


(Habari na Anita Balingilaki, Bariadi - Simiyu)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages