NEWS

Tuesday, 21 January 2025

ALAT yakagua miradi Tarime Mji, yataka inayoendelea kujengwa ikamilishwe kwa wakati



Wajumbe wa ALAT Mkoa wa Mara wakiongozwa na Mwenyekiti wao, Daniel Komote (wa pili kushoto mbele) kukagua ujenzi wa soko la kisasa la Tarime Mjini.
---------------------------------

Na Godfrey Marwa/ Mara Online News

Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) Mkoa wa Mara imekagua maendeleo ya ujenzi wa miradi mbalimbali katika Halmashauri ya Mji wa Tarime, na kutaka ikamilishwe kwa muda uliopangwa ili wananchi wapate huduma.

Miongoni mwa miradi iliyotembelewa na wajumbe wa ALAT Mara wakiongozwa na mwenyekiti wao, Daniel Komote leo Januari 21, 2025, ni ujenzi wa soko la kisasa la Tarime Mjini lenye thamani ya Shilingi bilioni 9.6.

Miradi mingine ni ujenzi wa jengo la kuhifadhi maiti na la wazazi katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime yenye thamani ya shilingi milioni 900. Pia, wametembelea Shule ya Sekondari Magena iliyojengwa kwa nguvu ya wananchi, Serikali Kuu na wadau wa maendeleo kwa gharama shilingi zaidi ya milioni 160.

Wakijadiliana jambo baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la kuhifadhi maiti.
-----------------------------------

Wajumbe hao wa ALAT wameipongeza halmashauri hiyo na Serikali Kuu kwa utekelezaji wa miradi mikubwa ya kijamii na kimkakati.

“Niungane wenzangu kupongeza Serikali ya CCM kwa ujenzi wa miradi hii. Ujenzi wa mradi (soko) unachochea uchumi, ningeomba mkandarasi ahakikishe anamaliza kazi kwa muda uliopangwa,” amesema Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Rorya, Gerald Samwel Ng'ong'a.

Kwa upande wake Komote ambaye pia Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Tarime na Diwani wa Kata ya Nkende, amewapongeza wananchi kwa kuendelea kushirikiana na serikali katika shughuli za maendeleo.

Komote ametumia nafasi hiyo pia kumwomba Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Gimbana Natavyo kutatua changamoto ya walimu wa kike katika shule za sekondari za pembezoni, ikiwemo Magena.
Read Also Section Example

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages