
Waziri wa Madini, Anthony Mavunde.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Serikali imetoa hati za makosa kwa kampuni 95 za uchimbaji mkubwa na wa kati wa madini kutokana na wamiliki wa leseni hizo kukiuka masharti ya leseni kama yalivyoainishwa kwenye Sheria ya Madini.
Akizungumza jana Mei 6, 2025 jijiini Dar es Salaam, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, alisema kampuni hizo zinapaswa kujibu hoja ndani ya siku 30, la sivyo zitafutiwa leseni zao.
Hati hizo za makosa zilitolewa rasmi Aprili 14, 2025 na muda wake utamalizika Mei 13, mwaka huu.
“Kama wanahoja walete majibu yao, tuyahakiki tukijiridhisha na hoja zao tutawaondolea makatazo, kama hawana hoja tutawafutia leseni zao kwa mujibu wa Sheria ya Madini Sura 123 ya utoaji na ufutaji wa leseni za madini na uchimbaji kifungu cha 63 na kanuni zake - ambacho kinaeleza ukipewa leseni unapaswa uanze kazi ndani ya miezi 18,” alisema Waziri Mavunde.
Alisema serikali ilitoa leseni kwa wachimbaji wa kati na wakubwa ambazo tangu kutolewa kwake hazijanyiwa kazi.
“Zipo Kampuni tangu zimechukua leseni mwaka 2011 mpaka leo hazijaingiza hata koleo kwenye eneo, miaka 14 sasa hazijaanza shughuli zozote, hatuwezi kuwa nchi ya namna hii.
Leseni saba tu kati ya 95 ukiziweka pembeni zina mtaji wa shilingi trilioni 15 zimelala, sisi hatuwezi kuwa nchi ambayo inatoa leseni kwa ajili ya kuchochea sekta ya madini kukua halafu kuna watu wanachukua leseni wanakaa nazo hawafanyii kazi kwa kisingizio kuwa tupo kwenye mazungumzo na serikali na sababu mbalimbali.
“Leseni za madini zikitolewa zina masharti nyuma yake kwenye ile karatasi hakuna sharti linalosema mtu ataanza uchimbaji wa madini nchini Tanzania akikamilisha mazungumzo na serikali, hiyo si sehemu ya sharti.
“Masharti ni kwamba mwombaji anapopewa leseni ni lazima aanze uchimbaji ndani ya miezi 18, vinginevyo awe na sababu ambazo zimeridhiwa na Waziri wa Madini kupitia Tume ya Madini, vinginevyo unapaswa kuanza uchimbaji ndani ya miezi 18,” alisisitiza Waziri Mavunde.
Aliongeza kuwa wale wote waliopata hati za makosa ambao wamejibu waende na barua ya ‘commitment’ ya kueleza wataanza uchimbaji lini, ambao katika barua hiyo pia ikitokea ameshindwa kukidhi kile alichosema kwenye barua sheria itafuata mkondo wake.
“Kuna vitu kama nchi ni lazima tuchukue maamuzi magumu, hatuwezi kuifanya nchi yetu mtu anakuja anachukua leseni halafu akaitafutie mtaji, sheria inataka mtu yoyote anayekuja kufanya maombi ya leseni lazima atoe uthibitisho wa uwezo wa kifedha na kiufundi kabla ya kupata leseni, sio nikupe ndio ukatafutie mtaji, maana yake utakuwa umekiuka masharti ya sheri kwa kutoa taarifa ambazo sio sahihi wakati wa kuomba leseni.
“Wale wote ambao hawatajibu ndani ya muda uliowekwa wasitegemee huruma yoyote, na wamekuwa ni mabingwa wa
kukimbilia mahakamani kuishtaki serikali, katika hili serikali imefuata taratibu zote kwa mujibu wa sheria inayowataka waliopata leseni kufanya uendelezaji wa leseni zao,” alisema Waziri huyo wa Madini.
Sekta ya madini ni kati ya sekta zenye mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi, hivyo shughuli za uchimbaji wa madini huchochea maendeleo makubwa ya kiuchumi.
No comments:
Post a Comment