NEWS

Saturday, 25 October 2025

Uzinduzi Umoja wa Wanahabari Tarime wafana, DC Gowele awachangishia zaidi ya milioni 11/-



Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele (kushoto), akimkabidhi Mwenyekiti wa Umoja wa Kuwezesha Waandishi wa Habari (REU), Jacob Karoli mchango wa kutunisha mfuko wa umoja huo katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika kwenye ukumbi wa CMG Hotels juzi Oktoba 24, 2025.

Na Christopher Gamaina
Tarime
-------------

Mkuu wa Wilaya (DC) ya Tarime, Meja Edward Gowele, ameongoza harambee ya kutunisha mfuko wa Umoja wa Kuwezesha Waandishi wa Habari (REU) wilayani humo, ili kuwawezesha kuboresha maisha yao na kutekeleza majukumu yao kwa weledi na ufanisi zaidi.

Harambee hiyo, iliyofanyika CMG Hotels mjini Tarime juzi Ijumaa, ikiwakutanisha wadau mbalimbali, wakiwemo watumishi wa serikali, wanasiasa, wafanyabiashara, taasisi za umma na binafsi.

Kupitia tukio hilo, shilingi zaidi ya milioni 11 (taslimu na ahadi) zilipatikana, ambapo DC Gowele alichangia shilingi 650,000, huku wana-REU wenyewe wakijichangia shilingi milioni 2.16.

Wengine walioshiriki na kiasi cha fedha walizotoa kikiwa kwenye mabano ni Mkurugenzi wa Chichake Sports Bar and Grill, Nicolaus Mgaya Chichake (milioni 1.5), Soya One limited (milioni moja) na Mwenyekiti Mstaafu wa CCM Mkoa wa Mara, Samwel Kiboye “Namba tatu” (milioni moja).


Mkurugenzi wa Chichake Sports Bar and Grill, Nicolaus Mgaya Chichake, akizungumza katika hafla hiyo.

Chama Kikuu cha Ushirika cha Wakulima wa Mara - WAMACU Ltd (500,000), Alikos Elution Plant (500,000), Mgombea Ubunge Jimbo la Tarime Mjini, Dkt. Mzarifu Zakaria kupitia CHAUMMA (500,000) na Mkurugenzi wa Moregas Primary English Medium (500,000).

Wengine ni Mbunge aliyepita, Michael Kembaki, Mgombea Ubunge Jimbo la Tarime Vijijini, Mwita Waitara na Mgombea Ubunge Viti Maalum Mkoa wa Mara, Ghati Chomete - wote kupitia CCM ambao kila mmoja aliahidi kuchangia shilingi 500,000.

Wadau wengine ni Benki ya CRDB Tarime, Godfrey Kisase Nkaina, TAKUKURU Tarime, Simion Kiles, Mkurugenzi wa Mara Online na Mgombea Udiwani Kata ya Sabasaba kupitia CHAUMMA, Butiku Masaku “Kapanga".

Wengine ni Mama Leah Hardware, Benki ya NBC Tarime, Mgombea Udiwani Kata ya Gwitiryo, Isaya Sangai “Tobiko”, Edward Empire, Bogomba Rashid, Veronica Nyagiro na Mwenyekiti UWT CCM Tarime.

DC Gowele aliwashukuru wadau wote waliohudhuria uzinduzi wa REU na kumuunga mkono kwa michango ya fedha kwa ajili ya kutunisha mfuko wa umoja huo.

“Niwapongeze wadau wote mlioitika kuja kuwashika mkono ndugu zetu waandishi wa habari. Wananchi wanategemea kalamu zao kuweza kujua dunia inavyokwenda. Hivyo, wawe sehemu ya kuandika vitu ambavyo vitalinda uhuru wetu, utamaduni wetu na maadili yetu,” alisema.

Alisisitiza kuwa waandishi wa habari ni mhimili muhimu katika maendeleo ya taifa, wakiwa daraja kati ya serikali na wananchi katika kuibua changamoto zilizopo kwa lengo la kuhamasisha na kujenga maendeleo jumuishi.

“Waandishi wa habari ni mkono wa serikali. Kama mkuu wa serikali kwenye wilaya mmekuwa mkinipa ushirikiano mkubwa, na wakati mwingine mmekuwa mkiibua changamoto zilizopo kwenye jamii, inatusaidia kutoka kwenda kuzishughulikia,” alisema.

Hivyo, aliwapongeza waandishi wa habari wa wilayani Tarime kwa mchango wao mkubwa katika kuhabarisha jamii kwa kuzingatia misingi ya uzalendo, kulinda amani na umoja.


Mgeni Rasmi, DC Meja Gowele alikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa REU.

Akizungumzia REU, DC Gowele aliwapongeza wanahabari hao kwa kuona umuhimu wa kuanzisha umoja huo, akiutaja kama chombo muhimu kitakachowezesha kurekebishana na kuboresha maisha yao.

“Niwapongeze waandishi wa habari kwa maamuzi yenu ya kujiunga ili muwe kitu kimoja - kama platform nzuri ya ninyi kushauriana, lakini pia kuimarisha maisha yenu na kazi zenu, hongereni sana,” alisema na kuendelea:.

“Naamini umoja huu utakuwa platform nzuri ya ninyi kujadiliana na kushauriana namna ya kufanya kazi na jamii zetu, wawekezaji, taasisi za umma na binafsi. Tunaamini mtakuwa mnajifunza kwa kuelezana ‘hapa mwenzetu uliteleza – rekebisha hapa’.

“Mkiandika jambo litakaloleta taharuki mnaweza mkawa chanzo cha matatizo katika wilaya yetu. Tujikite zaidi kwenye kutangaza mazuri yaliyopo Tarime, tunayo mazuri mengi sana ya kuandika.”

DC Gowele aliwakumbusha wanahabari kuwa uhuru wa vyombo vya habari una mipaka na kwamba kalamu zao zinapaswa kuwa chombo cha kujenga, si kubomoa. “Usiandike stori kwa ajili ya kumwangamiza mtu, andika kwa manufaa ya jamii,” alisema.

“Mkifanya balancing kwenye stories zenu hamtaingia migogoro na watu - hamtaingia migogoro na wawekezaji, hamtaingia migogoro na serikali. Uhuru wa vyombo vya habari ni mkubwa lakini lazima tutambue una mipaka,” alisisitiza DC Gowele.

Pia, aliwashauri kujenga uhusiano na wadau wa maendeleo, wakiwemo wawekezaji, taasisi za umma na binafsi, akitaja mifano ya taasisi zinazochangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi wa Tarime kama Chichake Sports Bar and Grill, Soya One Limited, CMG Hotels, WAMACU Ltd, Alkos Elution Plant na benki, zikiwemo, CRDB, NBC na NMB.

Aligusia sekta ya kilimo akisema Tarime imebarikiwa kuwa na misimu miwili ya mvua kwa mwaka na kwamba juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, zilizowezesha ujenzi wa soko la kisasa la mazao eneo la Regicheri, ni kielelezo cha dhamira ya serikali katika kuboresha maisha ya wananchi.

Kuhusu vivutio vya utalii, alisema wilaya ya Tarime inabeba sehemu kubwa ya Hifadhi ya Taifa Serengeti, likiwemo eneo maarufu la Kogatende ambako makundi ya nyumbu huvuka Mto Mara kwenda nchi ya Kenya na Kurudi Tanzania kila mwaka.

DC Gowele alisema eneo hilo linastahili kutangazwa zaidi ili kuongeza idadi ya watalii na kukuza uchumi wa Tarime.

“Maajabu ya dunia yako pale [Kogatende]. Tutumie kalamu zetu kutangaza mazuri hayo, ni kivutio kikubwa kwenye wilaya yetu. Lakini pia kuna wawekezaji wakubwa wako pale. Kwa hiyo, mzunguko mkubwa wa fedha uko katika wilaya yetu,” alisema.

Mkuu wa Wilaya, Meja Gowele, alisisitiza pia umuhimu wa waandishi wa habari kujiendeleza kitaaluma ili kuongeza weledi wao katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Elimu haina mwisho, mimi mpaka sasa ninasoma. Kwa hiyo, hata ninyi kwenye tasnia yenu mjiendeleze ili mfanye vizuri zaidi,” alisema DC Gowele.

Aliwahakikishia waandishi wa habari kuwa serikali itaendelea kushirikiana nao kwa karibu katika kuhakikisha wanafanya kazi zao kwa uhuru, lakini ndani ya mipaka ya kisheria na maadili ya taaluma.

“Mimi kama mkuu wa serikali kwenye wilaya nitahakikisha taasisi zote za umma zinawapa ushirikiano pale mtakapohitaji, na mkikwama basi tuwasiliane, kama ni taarifa ambayo hairuhusiwi utaambiwa,” alisema.

Alihitimisha hotuba yake kwa kutoa wito wa kuwataka wananchi kuepuka uchochezi na uzushi kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29, 2025, akisema serikali imejipanga kuhakikisha unafanyika katika mazingira ya amani, utulivu na usalama.

“Tunatahadharisha wananchi kuepuka uchochezi na uzushi, ikiwemo kupitia mitandao ya kijamii. Watu wajitokeze kwa wingi kutumia haki yao ya kikatiba kuchagua viongozi. Niwahakikishie tutafanya uchaguzi katika mazingira ya amani na utulivu kwani serikali tumejipanga vizuri,” alieleza.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa REU, Jacob Karoli, alimshukuru DC Gowele na wadau wote kwa kukubali kuunga mkono umoja huo na kuwaahidi ushirikiano wa dhati katika utekelezaji wa shughuli za ujenzi wa taifa.


Naye Jacob Mugini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Mara, aliwapongeza wana-REU akisema hatua hiyo ni mwelekeo mzuri wa katika kujiinua kiuchumi.

“Ningependa kuona juhudi kama hizi zinafanywa na waandishi wa habari katika kila wilaya ya mkoani Mara,” alisema Mugini ambaye pia ni mmiliki wa Gazeti la Sauti ya Mara na Blogu ya Mara online News.

Kwa upande wao, wadau walioshiriki hafla hiyo waliahidi kuendelea kushirikiana na waandishi wa habari katika kujenga wilaya ya Tarime kijamii na kiuchumi.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages